NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 15, 2012

60 Serikalini kuhakikiwa mali zao,Sitta ndani

TUME ya Maadili ya Viongozi wa Umma imeanza mchakato wa kuhakiki mali za viongozi wa umma nchi nzima ambapo kwa awamu ya kwanza itaanza na vigogo 60 akiwamo Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta na Waziri Samia Suluhu Hassan wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano).  Wengine ni wakuu wa mikoa na wilaya, Meya wa majiji, madiwani, wabunge na wakurugenzi wa taasisi mbalimbali za Serikali.

 Zoezi la uhakiki wa mali za viongozi hao litaanza Februari 20 hadi Machi mosi mwaka huu ambapo linafanyika baada ya kukamilika kwa zoezi la urejeshaji wa fomu za utajaji mali na madeni kutoka kwa watumishi mbalimbali wa Serikali.   Mbali na Sitta ambaye pia ni Mbunge wa Urambo Mashariki, wabunge wengine watakahakikiwa mali zao katika awamu hiyo ni John Mnyika(Ubungo), Joseph Mbilinyi (Mbeya Mjini), Jerome Bwanansi (Lulindi), Faith Mitambo (Liwale) na Stella Manyanya (Viti Maalum).

Katika orodha hiyo yumo pia Meya wa Jiji la Mbeya Athanas Kapunga, Mkuu wa Mkoa wa Lindi Ludovock Mwananzila, Meya wa Jiji la Dar es Salaam Didas Masaburi na Meya wa Jiji la Tanga, Guledi Mohamed.  Wengine ni  Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Charles Nyamrunda, Mkurugenzi Mkuu Shirika la Nyumba la Taifa(NHC), Nehemia Mchechu, Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Placidus Luoga na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Elaston Mbwilo.

  Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana Kamishna wa Tume ya Maadili, Jaji Mstaafu Salome Kaganda alisema kuwa uhakiki huo ni nguzo bora ya kuijenga jamii ya Watanzania, hasa viongozi wa umma katika kuishi kwa kufuata misingi ya uadilifu, iliyowekwa na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.  Alisema kwa kuwa idadi ya viongozi ni kubwa na kwamba  tume hiyo itaanza na uhakiki wa viongozi 60 wenye nyadhifa mbalimbali.

“Sisi tunachokiomba kutoka kwao ni kutoa ushirikiano wa kutosha kwa maofisa wetu  wakati wa zoezi zima la uhakiki wa mali zao,” alisema Kaganda.  Alisema wananchi wanatakiwa kushirikiana na tume hiyo kutoa taarifa zitakazowasaidia kugundua mali zilizofichwa, ambazo zinadhaniwa kuwa ni za viongozi wa umma wanaoguswa na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.   Aliwataka viongozi wanaohakikiwa kutokuwa na hofu kwa kuwa zoezi hilo ni la kawaida.

 “Hawa hawana tuhuma zozote ni utaratibu wa kawaida tu,”alisema.  Jaji mstaafu Kaganda aliliambia gazeti hili kuwa si kosa kwa kiongozi yoyote wa Serikali kuwa na mali na kwamba kosa  ni mali hizo kupatikana kinyume na sheria.  “Mbunge akiwa mfanyabiashara na biashara yenyewe inafuata sheria hilo sio tatizo ila tukigundua mali hizo au biashara inafanyika kinyume na sheria tunaweza kuwaeleza Takukuru" alisema Kaganda.

Alisema kuwa kwa sasa uadilifu kwa viongozi wa umma umeshuka hivyo zoezi kama hilo kwa kiasi kikubwa linaweza kurudisha uadilifu huo.  Katika hatua nyingine, Jaji Kaganda alisema anafanya utafiti wa sheria ya kutenganisha biashara na uongozi.  “Nafanya utafiti kuhusu sheria hii ila kwa sasa ni mapema mno kueleza nilipofikia,” alisema Kaganda.          

No comments:

Post a Comment