NJOMBE

NJOMBE

Sunday, February 19, 2012

KATIBU TAWALA MKOA SINGIDA AASA PROGRAMU ZA MAJI KUSIMAMIWA NA WATU WALIOFUNZWA VYEMA.


Katibu tawala mkoa wa Singida Liana Hassan akifungua mafunzo ya siku moja yaliyohudhuriwa na kamati ya seketarieti ya mkoa wa Singida na za halmashauri za wilaya ya Manyoni na Singida.
Mshauri mwandamizi wa Mrogramu ya usambazaji wa maji vijijini RUWASA-CAD Kazuyuki Suenaga akitoa taarifa yake mbele ya mkutano wa mafunzo yaliyohudhuriwa na kamati za maji na usafi wa mazingira ya seketarieti mkoa wa Singida na za halmashauri za wilaya ya Singida na Manyoni.
Baadhi ya wanakamati za maji na usafi wa mazingira za seketarieti ya mkoa wa Singida na halmashauri za Manyoni na Singida.(Picha zote na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu.
Katibu tawala mkoa wa Singida Liana Hassan amesema programu za maji zinazofadhiliwa na wafadhili mbali mbali, zitakuwa endelevu tu iwapo zitasimamiwa na watu waliofunzwa vema mbinu bora za uendeshaji wa miradi ya maji.
Akifungua mkutano wa siku moja wa kwanza uliohusu mafunzo ya kuzijengea uwezo timu za maji na usafi wa mazingira za sekretarieti ya mkoa na zile za halmashauri za wilaya ya Manyoni na Singida, Hassan amesema mafunzo hayo yanalenga kuzijengea uwezo timu hizo ili ziweze kusimamia vizuri utekelezaji wa usambazaji wa maji vijijini awamu ya pili (Rural water supply and sanitation capacity development -RUWASA – CAD).
 AKifafanua amesema watu/viongozi hao waliofunzwa vema juu ya uendeshaji bora wa miradi ya maji, watasaidia kuwafunza na kuwahamasisha  watumiaji wa maji, mbinu sahihi zitakazosaidia miradi yao ya  maji, kuwa endelevu.
Aidha, Katibu huyo wa mkoa amesema lengo letu sote ni kuhakikisha kuwa asilimia 48 ya wakazi wa mkoa wa Singida wanapata maji safi na salama kwa umbali mfupi kutoka wanakoishi.
Lengo hilo litafikiwa tu iwapo jamii itakuwa imeelimishwa mbinu ya kutunza miradi hiyo.
Katika hauta nyingine, Katibu tawala huyo amesema utekelezaji wa mradi wa usambazaji wa maji vijijini utakapoanza, uangalie uwezekano wa kusaidia kugharamia masomo ya ufundi wa pampu za maji na injini kwa vijana waishio vijijini, ili kuondoa uhaba mkubwa wa mafundi wa aina hiyo ngazi ya vijiji.
 Kwa upande wake mshauri mwandamizi wa mradi wa RUWASA – CAD awamu ya pili Kazuyuki Suenaga, amesema kwa sasa wanaendelea kuzijengea uwezo timu za maji na usafi wa mazingira za sekretarieti ya mikoa na za halmashauri za wilaya.
Suenaga asema timu hizo za mikoa ya Singida, Tabora na Mwanza, zitajengewa uwezo kwa kupatiwa mafunzo yanayohusu uendeshaji na utunzaji bora wa miradi ya maji.
Amesema wanayo imani kwamba baada ya kuzifunza timu hizo na zenyewe, zitafunza jamii ili miradi iliyopo kwenye maeneo yao iwe endelevu.
Aidha, Suenaga amesema kutokana na hitaji la Tanzania la uboreshaji wa sekta ya maji, serikali ya Japan imeamua kuiunga mkono kwa kusaidia kupatikanaji wa maji safi na salama na usambazaji wake, maeneo ya vijijini chini ya ushirikiano na program ya Japan International Co-operation Asency (JICA).

No comments:

Post a Comment