NJOMBE

NJOMBE

Thursday, February 2, 2012

Sumaye ang’ang’aniwa bungeni

MBUNGE wa Mvomero, Amos Makalla (CCM), amemtuhumu Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, kwamba amekwapua ekari 326 za shamba la ushirika la wilayani Mvomero lililopaswa kugawanywa kwa wanakijiji wa Mvomero, mkoani Morogoro.
Kutokana na hali hiyo, mbunge huyo alihoji utaratibu uliotumiwa na serikali kumuuzia Sumaye shamba hilo badala ya kuwapa wananchi kipaumbele.
Makalla alitoa tuhumu hizo jana wakati akiuliza swali bungeni katika kipindi cha maswali na majibu ambapo pia aliitaka serikali itoe tamko kuhusu shamba hilo kwakuwa Rais Jakaya Kikwete wakati wa kampeni zake mwaka 2010, aliwahi kuahidi kushughulikia kero hiyo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodluck Ole-Medeye, alisema kuwa shamba hilo lenye hati namba 21919, lililoko katika Kijiji cha Mvomero, Wilaya ya Mvomero, linamilikiwa na mke wa Sumaye, Esther Sumaye kihalali.
Alisema kabla ya shamba hilo kumilikiwa na Esther Sumaye, lilikuwa likimilikiwa na Onasaa Waryaeli Kisanga na Mesaki Josiah Ndanshau, wakitumia jina la Mvomero River Farm Limited kwa hati namba 211919.
Kwa mujibu wa naibu waziri huyo, kumbukumbu zilizoko kwenye wizara yake zinaonyesha kuwa awali shamba hilo lilikuwa likimilikiwa na Mvomero River Farmers Limited ya Morogoro kuanzia mwaka 1978 hadi Julai 1985 lilipohamishiwa kwa Kampuni ya Wami & Magole Farmers Co-operative Society ya Morogoro.
Alisema Machi 1966 Kampuni ya Wami & Magole Farmers Cooperative Society Limited, ilibadili jina na kuitwa Morogoro Farmers Primary Society Limited.
“Aidha, tarehe 27, Novemba 2001, Morogoro Farmers Primary Co-operatives Ltd, walimuuzia Esther Sumaye shamba hilo na baada ya kukamilisha taratibu zote za kisheria ikiwa ni pamoja na kulipa ushuru kwa serikali, uhamishwaji wa miliki ulikamilishwa mwaka 2002 kwa mujibu wa kifungu cha 61 cha sheria ya ardhi namba 4 ya mwaka 1999,” alisema naibu waziri.
Kwa kuwa Esther Sumaye ana miliki shamba hilo kihalali na kuliendeleza kwa kuzingatia masharti ya hatimiliki, waziri alisema serikali inaheshimu haki zake na kwenye ibara ya 24 (1) na (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977.
Alisisitiza kuwa kwa kuwa mwenye shamba aliamua kumuuzia Sumaye na kuwanyima wananchi, serikali inaheshimu haki hiyo na kuongeza kuwa shamba hilo ni mali ya Sumaye.
Kwa muda mrefu sasa, Sumaye na Rais mstaafu, Benjamin Mkapa wamekuwa wakilalamikiwa kujitwalia maeneo makubwa ya ardhi kifisadi mkoani Morogoro, hivyo wananchi wa eneo hilo wamekuwa wakiomba serikali iwapokonye vigogo hao na kuligawa kwa wananchi.
Hata hivyo Sumaye amepata kujitokeza hadharani mara nyingi kupinga madai kwamba amepora ardhi hiyo na badala yake amekuwa akisisitiza kuwa ana miliki kihalali.

No comments:

Post a Comment