NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 1, 2012

Mgomo wa madaktari kutikisa Bunge leo


SERIKALI leo inatarajia kutoa kauli bungeni juu ya hatma ya mgomo wa madaktari unaoendelea nchini ambapo umedumu kwa wiki mbili sasa.
Akizungumza kabla ya kuahirisha shughuli za Bunge jana, Spika wa Bunge, Anna Makinda, alisema kuwa serikali imeshapata maombi kwa ajili ya kutoa kauli  juu  ya mgomo huo ulioleta athari kubwa nchini.
Spika alitoa kauli hiyo wakati akijibu mwongozo wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, aliyetaka kujua serikali inatoa kauli gani juu ya mgomo wa madaktari nchini.
Zitto aliitaka serikali kutoa kauli juu ya mgomo huo pia ni lini madaktari hao wangelipwa haki zao.
Akijibu hoja hiyo Makinda alisema kuwa tamko la serikali litatolewa leo na hali hiyo inatokana na kuwepo kwa utaratibu unaotaka kauli ya serikali katika suala hili, upitie kanuni na taratibu za kibunge.
“Kwa kuwa serikali ilishapokea maombi ya kutoa tamko ni lazima waziri aandike tamko hilo na kulichapisha ili anapolisoma bungeni, liwe limeandikwa na liweze kusomwa na wabunge wote,” alisema.
Mbali na hilo alisema ni lazima pia tamko hilo lipitie katika kamati ya uongozi ya Bunge ili liweze kujadiliwa na baada ya hapo, litapelekwa kwa Spika na kutoa baraka za kuileta bungeni.
Wakati serikali ikijiandaa kutoa tamko bungeni, tayari serikali hiyo hiyo kupitia kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda ilishatoa kauli na kuwapa madaktari hao saa 24 warejee kazini, vinginevyo wahesabu kwamba wamejifuta kazini.
Pamoja na tamko hilo la vitisho, bado madaktari hao wameendelea na mgomo wao hadi jana na vifo vingi vimeripotiwa kutokea sehemu mbalimbali nchini kutokana na mgomo huo.

No comments:

Post a Comment