NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 1, 2012

Halmashauri Singida zaongoza kwa rushwa

HALMASHAURI za wilaya na manispaa mkoani Singida zimeendelea kuongoza kwa matukio 58 dhidi ya malalamiko 85 ya kuomba na kupokea rushwa katika kipindi cha mwaka jana.
Halmashauri hizo ambazo zinadaiwa kuwa zimejaa wabadhirifu wa mali za umma, zimeongoza kwa kulalamikiwa kwa matukio hayo ikiwa ni asilimia kubwa ikilinganishwa na ofisi nyingine.
Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Singida, Julliane Kallasa, alisema jeshi la polisi linashika nafasi ya pili kwa kuripotiwa kuwa na matukio tisa.
Alitaja taasisi nyingine na idadi ya malalamiko yake yakiwa kwenye manbano kuwa ni mahakama (1), taasisi binafsi (7) na taasisi zinginezo (10).
Alisema vitendo vya kuomba na kupokea rushwa kwa mwaka jana, viliongezeka na kufikia 85 tofauti na mwaka juzi ambapo zilikuwa 80.
Pamoja na mambo mengine alisema mwaka jana jumla ya kesi nne zilifunguliwa mahakamani ikilinganishwa na kesi mbili za mwaka juzi.
“Kesi moja ilitolewa hukumu mwaka jana ambapo mtuhumiwa Elipharaja Hamisi  Omari, Ofisa Mtendaji wa kijiji cha Shati wilayani Iramba, alipatikana na hatia ya kuomba na   kupokea rushwa. Alihukumumiwa adhabu ya kutumikia jela miaka mitatu,” alisema Kallasa bila kutaja aina ya rushwa na kiasi alichopokea mshtakiwa.
Mkuu huyo wa Takukuru alisema katika kesi zingine mbili za watuhumiwa Wilson Ngasa Gasule toka sekretarieti ya mkoa wa Singida na Gerwin Lyaheja toka ofisi ya mkuu wa wilaya, hawakupatikana na hatia na waliachiwa huru na mahakama ya mkoa.
Akifafanua, alisema washtakiwa hao walikuwa wakikabiliwa na tuhuma za kutumia nyaraka ili kumdanganya mwajiri wao wajipatie fedha, kitendo ambacho ni kinyume na sheria no.22 ya PCCA ya mwaka 11/2011.
“Pia mtuhumiwa Khalifa Abdala Kisumo, ofisa tabibu wa hospitali ya mkoa wa Singida, naye aliachiliwa huru na mahakama baada ya kushahidi kushindwa kumuunganisha na kosa la kuomba na kupokea rushwa,” alisema.
Alitoa wito kwa viongozi na watendaji katika mkoa wa Singida kusimamia vizuri rasilimali za umma ili zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa.

No comments:

Post a Comment