NJOMBE

NJOMBE

Tuesday, July 10, 2012

SHIRIKA LA MAENDELEO BUMBULI

 

Taarifa kwa Vyombo vya Habari
Napenda kuwatangazia wana-Bumbuli kwamba ile ahadi niliyotoa wakati wa kampeni – ahadi ya kuanzisha Shirika la Maendeleo Bumbuli – imetimia. Shirika limepata usajili, limefungua ofisi, lina watumishi wa mwanzo na tayari ipo miradi minne ambayo utekelezaji wake utaanza mara moja. Tutazindua Shirika hili tarehe 4 Agosti 2012, katika mkutano wangu na wana-Bumbuli waishio Dar es Salaam na mikoa ya jirani, na baadaye katika mikutano na wananchi jimboni Bumbuli.
Chimbuko
Nilipoamua kugombea Ubunge wa Bumbuli mwaka 2010, niliamua kwamba katika utumishi wangu kama Mbunge nitashirikiana na Wana-Bumbuli pamoja na marafiki na washirika wa maendeleo wa ndani na nje ya nchi katika kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii Bumbuli. Jimbo letu ni kati ya majimbo yaliyo nyuma kimaendeleo kwa kiasi kikubwa na hivyo kuhitaji jitihada za ziada – zaidi ya zile za Serikali. Katika kufikia lengo hilo, niliahidi kuanzisha Shirika litakaloratibu shughuli za maendeleo katika Jimbo.
Nilifikia uamuzi wa kuanzisha Shirika nikitambua kwa dhati uwepo wa jitihada nzuri za serikali katika kuboresha maisha ya watu wa Bumbuli nikitegemea pia serikali kuendeleza jitihada zaidi. Hata hivyo natambua kwamba kazi ya maendeleo si kazi ya serikali pekee, inahitaji ushiriki wa kila mmoja na hasa sekta binafsi ili kuisadia juhudi za serikali kufikia malengo ya maendeleo. Nilitaka kuchambua uwezo wa watu binafsi, wafanyabiashara na taasisi mbalimbali katika kupanua wigo wa ajira na shughuli za kipato kwa watu wa Bumbuli kupitia uwekezaji katika jamii.
Mpango wa Mageuzi Bumbuli
Mpango huu ulitokana na mawazo niliyokuwa nayo nilipoamua kugombea ubunge juu ya haja kuunganisha jitihada za wenyeji wa Bumbuli, wafanyabiashara na taasisi za hapa nchini, na wawekezaji kutoka nje katika kufanikisha mageuzi ya kijamii na kiuchumi. Niliamini jitihada za sekta binafsi zikioana na mipango ya maendeleo ya serikali kutachochea kasi ya ukuaji wa uchumi wa wana-Bumbuli na hivyo kupanua wigo wa ajira na shughuli za kibiashara za uzalishaji mali katika Jimbo.
Malengo ya mpango wa kuikwamua Bumbuli kupitia uwekezaji katika jamii ni kama ifuatavyo:
1. Kuongeza pato la wakulima wa Bumbuli kutokana na mazao wanayovuna kwa kuboresha mbinu za kilimo, mbinu za kuhifadhi mazao, na hatua mahsusi za kuongeza thamani ya mazao hayo (value-addition).
2. Kuwavutia wawekezaji kujenga taasisi au shule itakayokuwa na wanafunzi, walimu na wafanyakazi wengine watakaotumia bidhaa zinazozalishwa Bumbuli, hivyo kutengeneza ajira na fursa za kujiongezea kipato kwa wananchi.
3. Kuleta huduma za kifedha kwa kuanzisha taasisi ya fedha Bumbuli ambayo hatimaye itakuwa benki ya wananchi wa Bumbuli ambayo itatoa mikopo kwa masharti nafuu.
4. Kuchukua hatua mahsusi za kuhifadhi mazingira ya Milima ya Usambara kwani maisha na maendeleo ya kiuchumi ya watu wa Bumbuli yanategemea sana mazingira na mandhari ya milima ya Usambara.
5. Kuanzisha Shirika la Maendeleo Bumbuli litakalokuwa na jukumu la kubuni, kuratibu na kusimamia uendeshaji wa shughuli zilizoainishwa hapo juu. Shirika hili ndilo litakalokuwa kiini cha mtandao wa kijamii wa uchumi kwa Bumbuli.
Malengo haya yamekusudiwa kuwanufaisha wananchi kwa kuanzisha mtandao wa kimataifa wa kibiashara ambapo wadau mbalimbali watashiriki; na hatamu za uchumi zikishikiliwa na watu wa Bumbuli wenyewe.
Shirika la Maendeleo Bumbuli
Shirika la Maendeleo ya Bumbuli ni shirika la maendeleo lisilotengeneza faida lenye lengo la kukuza uchumi na kuchochea maendeleo ya Jimbo. Shirika hili limesajiliwa kama kampuni yenye ukomo wa dhamana, na litafanya biashara ili kulipia gharama za uendeshaji na faida inayopatikana itatumika kugharamia miradi ya maendeleo ili kufikia malengo ya kijamii ya Mkakati wa Mageuzi ya Uchumi wa Bumbuli. Shirika litakuwa na kazi zifuatazo;
1. Kuihamasisha sekta binafsi kushiriki katika maendeleo ya Bumbuli kwa kuwekeza katika maeneo mblimbali. Uwekezaji huu utahusisha wafanyabiashara wa ndani na wale wa kigeni na Shirika litajihusisha zaidi katika kutoa msaada wa kitaalamu, na kuratibu mtandao wa kibiashara utakaoenea kuanzia ngazi ya wilaya, taifa na kimataifa.
2. Kubuni na kuitangaza ‘Chapa Lushoto’ (Lushoto Brand) pamoja na kutayarisha mafunzo kwa wakulima juu ya kutayarisha mazao yao ili yapate kuwa na thamani bora zaidi. Shirika hili litajenga mfumo utakaosaidia kununuliwa kwa mazao ya wakulima na masoko ya bidhaa, muundo utakaotumiwa na wafanyabiashara binafsi.
3. Kuvutia uwekezaji kwa njia ya kuitangaza Bumbuli pamoja na kuishauri halimashauri na serikali za mitaa kuhusu maeneo ya kuwekeza na miundombinu ya kuboresha ili kuvutia uwekezaji zaidi.
4. Kutafuta fedha kwa ajili ya uwekezaji wa kijamii na kibiashara na kutoa msaada wa kihuduma kwa makampuni ya biashara ya nyumbani na uwekezaji wa kutoka nje.
5. Kuratibu mipango ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya wadau mbalimbali wa maendeleo Bumbuli.
6. Kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika mpango wa Maendeleo na Mpango wa uwekezaji.
Shirika litaongozwa na bodi itakayokuwa na watu kati ya nane na kumi na moja na kuendeshwa na timu ya watu watano ambao watakuwa ni, Mkurugegenzi Mtendaji, Mweka Hazina, Wachambuzi wawili na Mhasibu.
Miradi ya Mwanzo ya Shirika la Maendeleo Bumbuli
1. Mradi wa Kituo cha Kukusanya, Kusafisha, Kugredi, Kupaki na Kutafuta Masoko ya Mboga na Matunda ya Bumbuli (Bumbuli Packing House)
Wilaya ya Lushoto, jimbo la Bumbuli likiwemo, inasifika kwa kilimo cha mboga na matunda. Hata hivyo, asilimia hamsini (50%) ya mboga na matunda yanayolimwa Bumbuli yanaharibika – kwa kutokufika sokoni au kutopata soko la uhakika. Hata yale mazao yanayonunuliwa, wakulima wanapata mapato kidogo sana ambayo hayaendani na thamani ya jasho lao.
Mradi wa Bumbuli Packing House, ambao utajiendesha kibiashara, una dhamira ya kumaliza tatizo hili. Pamoja na hili mradi huu utawawezesha wakulima kwa pembejeo – mbegu, mbolea, pampu, nk – na mafunzo ili wazalishe mboga na matunda bora zaidi ya kukidhi mahitaji ya soko la kimataifa.
Mradi huu, katika awamu ya kwanza, utagharimu shilingi milioni 780. Utafiti wa Kibiashara (Market Analysis Survey) umefanyika, Andiko la Kibiashara limekamilika. Na majadiliano na wadhamini kupata fedha hizi yamefikia mwisho ambapo ndani ya mwezi mmoja fedha hizo zitapatikana, na baada ya maandalizi kukamilika (ikiwemo kupata professional management), mradi utaanza.
2. Mradi wa Kiwanda cha Kusindika Mboga na Matunda
Shirika liko katika hatua za mwisho za mazungumzo ya kukifufua upya kiwanda cha kusindika Mboga na Matunda (Natural Choice) kilichopo Soni, jimbo la Bumbuli, ambacho mwanzoni kwa miaka ya 2000 kilikuwa na sifa kubwa ya kutoa bidhaa nyingi, bora na za thamani kubwa.
Mradi huu utaenda hatua ya mbele zaidi ya Bumbuli Packing House kwa kutengeneza juisi, jams, concentrates na bidhaa nyingine za mboga na matunda kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi. Mradi huu, sio tu utatoa ajira kwa watu wa Bumbuli, bali pia utahakikisha soko la uhakika kwa mboga na matunda ya Lushoto linapatikana na kuongeza thamani ya mazao ya wakulima na hivyo kuwaongezea kipato.
3. Mradi wa Kutoa Mikopo kwa Masharti Nafuu (Bumbuli Microfinance Institutition)
Jimbo la Bumbuli halina tawi la benki yoyote na huduma ya fedha ni tatizo kubwa. Shirika la Maendeleo Bumbuli limeomba leseni kutoka Benki Kuu kuanzisha taasisi ya fedha kwa ajili ya ukopeshaji kwa masharti nafuu na pamoja na huduma nyingine za fedha. Andiko la Mradi huu limefanywa kitaalam sana, baada ya utafiti wa karibu miezi nane kuhusu njia muafaka ya kutoa huduma ya fedha kwa masharti nafuu kwa watu wa Bumbuli. Mradi huu utagharimu shilingi milioni 450 kwa kuanzia na baada ya miaka mitatu mtaji utaongezwa na kufikia shilingi bilioni 1.6. Wakati tunasubiri usajili na leseni kutoka Benki Kuu tayari wapo wafadhili ambao, baada ya kusoma andiko letu, wameonyesha nia ya kusaidia mradi huu.
Msingi wa mradi huu ni kuwezesha vikundi vya kuweka na kukopeshana fedha ambavyo tayari vipo lakini vina mtaji mdogo, kutoa mafunzo ya fedha kwa vikundi hivi, na kuhamasisha kuanzishwa kwa vikundi vingine. Kipaumbele na nafuu ya mikopo itatolewa zaidi kwa vikundi vitakavyotumia fedha hizi kwa uzalishaji mali na shughuli ambazo zitaajiri watu wengine.
4. Mpango wa Malipo kwa Kufanya Vizuri kwa Shule za Sekondari (Cash-On-Delivery for Secondary Education in Bumbuli)
Shirika la Maendeleo Bumbuli (BDC) litakavyotekeleza program ya msaada ya Malipo kwa kufanya vizuri** au cash on delivery (COD), ambayo itaongeza umakini na tija kwenye kujifunza na matokeo ya mitihani katika shule za sekondari jimboni Bumbuli. Kulingana na utafiti wetu, jimbo la Bumbuli liko kwenye hali ya kukata tamaa ya kupata msaada kwenye Sekta yake ya Elimu ya Sekondari. Shirika la Maendeleo Bumbuli (BDC) litatekeleza program ya majaribio ya malipo kwa kufanya vizuri (COD), ya miaka mitatu ambayo itafanya malipo kulingana na idadi ya wanafunzi ambao wamefaulu Mitihani ya Taifa ya Kidato cha Nne. Shirika la Maendeleo Bumbuli (BDC) linalenga kuboresha matokeo ya kujifunza/elimu katika jimbo la Bumbuli kupitia program hii ya kutoa motisha. Program hii itahusu Shule za Sekondari za Serikali za Kata.
Malipo kwa kufanya vizuri (COD) ni utaratibu mpya kutoa msaada ambapo wafadhili hutoa pesa kwenye maendeleo yanayopimika kwa kuangalia matokeo maalum. Unahusianisha moja kwa moja malipo na matokeo maalum, ikiwapatia watendaji/wapokeaji motisha ya kuongeza nguvu zao za kufanyakazi ili kufikia maendeleo.
Msingi na uhalali wa wazo la CDO, ulioanzishwa awali na Kituo cha Maendeleo ya Kimataifa(Center for Global Development) mjini Washington, umejikita kwenye mtazamo kwamba kazi za maendeleo ni lazima zitathminiwe kwenye athari (impact) zinazoletwa. Mbinu inawakilisha mabadiliko kutoka kufuatilia nguvu na rasilimali ambavyo mashirika huwekeza katika kutoa misaada - 'nyenzo/rasilimali', na pia shughuli na vifaa/vitendeakazi vinavyotokana na uwekezaji huo - 'matokeo'. Badala yake, mbinu hii inalenga kujikita kuangalia namna gani maisha ya watu masikini yameweza kubadilishwa kutokana na uwekezaji kwenye sekta au eneo fulani la maendeleo (afya, elimu, n.k).
Mnamo mwezi Septemba 2011, Shirika la Maendeleo Bumbuli lilifanya utafiti wa kina juu ya mazingira ya kujifunzia Bumbuli na kugundua kwamba shule nyingi, walimu, na wanafunzi wa Bumbuli hawana motisha wala rasilimali zinazohitajika kuwawezesha wafanye vizuri kama inavyotarajiwa.
Kwa wastani, kila shule iliyotoa data za matumizi ya pesa ilionyesha ni Sh. 5,268 kwa kila mwanafunzi kwa mwaka 2010 (kiasi kilichotarajiwa kwa shule za Sekondari ni shilingi 25,000 kwa kila mwanafunzi). Pamoja na hayo, utafiti ulionyesha kuwa ni 71% tu ya walimu walikuwepo shuleni, ambapo ni 19% tu walikutwa madarasani. Utafiti huo ulionesha kuwa walimu hupata mishahara yao kwa wakati. Wastani wa mshahara halisi wa mwalimu wa Bumbuli ni Sh.395,000 kutoa malipo ya deni ya Sh.74,000 kila mwezi. Wengi walionesha kuwa na shughuli ya ziada ya kiuchumi (67%), hasa kilimo (90%). Wengi wao (98%) walidai kutokuhusishwa katika hatua za kupanga bajeti za shule. Wastani wa Pato la Mtanzania anayeishi kijijini (ikiwemo Bumbuli) ni Sh.152,000 (HBS, 2010). Wakati 89% ya wanafunzi wanaonesha kushiriki katika shughuli za kiuchumi wa familia, bado 70% wanafanikiwa kupata muda kidogo wa kukamilisha kazi zao za masomo wakiwa nyumbani, huku 34% inaonesha hawakufika shule kwa mwezi uliopita kutokana na kusaidia shughuli za nyumbani. Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne ya mwaka 2011 kwa Shule za Bumbuli yalikuwa mabaya sana. Kati ya wanafunzi 1,327 waliofanya mtihani, hakuna aliyepata Division 1, waliopata Division 2 ni wanne, waliopata Division 3 ni 39, na waliobakia, yaani wanafunzi 1,274, walipata Division 4 na 0.
Pamoja na hatua mahsusi ambazo Serikali inachukua kuboresha elimu nchini na kuongeza ufaulu, Shirika la Maendeleo Bumbuli, kupitia Program hii ya COD, linataka kuonesha kwamba fedha zinaweza kugawika vizuri na kwa usahihi ili kuboresha elimu kwa kupima kiwango cha ufaulu wa wanafunzi.
Hatua na mikakati inayopendekezwa
Program ya COD kwa Shule za Sekondari Bumbuli itahusisha makubaliano kati ya Shirika la Maendeleo Bumbuli, Shule za Sekondari Bumbuli na Halmashauri ya Wilaya kulipa jumla ya kiasi cha Dola za kimarekeni 100 kwa kila mwanafunzi anayefaulu mitihani ya kidato cha IV kwa daraja la I-III. Malipo ya COD yatafanyika baada ya uthibitisho wa matokeo ya mtihani wa kidato cha nne. Fedha zitapelekwa Halmashauri ya Wilaya, Shule za Sekondari na kwa walimu na wanafunzi. Fedha zitakazogawiwa kwa shule zitatumika kwa ajili ya mahitaji ya kielimu ya shule kama zilivyowekewa vipaumbele na Bodi za Shule.
Watakaonufaika na mradi:
Kwa kila mwanafunzi atakayefaulu mtihani (Div I-III) anapomaliza kidato cha nne, Shirika la Maendeleo Bumbuli kupitia program ya COD litatoa malipo yafuatayo:
1. Walimu: Tsh 60,040/= kwa kila mwanafunzi anayefaulu mtihani
2. Wanafunzi: Tsh 50,500/= Kwa kila mwanafunzi anayefaulu mtihani
3. Shule: Tsh 31,600/= Kwa kila mwanafunzi anayefaulu mtihani
4. Halmashauri ya Wilaya: Tsh 15,800/= kwa kila mwanafunzi anayefaulu mtihani
Vipimo na Ukaguzi:
Data za mitihani kuanzia mwaka 2011 zitatoa msingi wa awali, na msingi huo utakuwa ukibadilishwa kila mwaka na ufanisi wa utendaji wa shule, hivyo kila mwaka unakuwa msingi kwa ajili ya malipo ya mwaka ujao wa. Kiashiria cha matokeo kitakuwa idadi ya wanafunzi ambao wamefaulu kidato cha nne kwa kupata daraja la I-III. Ili kuyadumisha matokeo hayo, hatua mbalimbali zitakuwa vikiripotiwa kila mwaka na shule na halmashauri. Mkataba, matokeo, na taarifa nyingine zitawekwa wazi kwa wananchi ili kuongeza uwajibikaji wa wafadhili na wapokeaji
Shirika la Maendeleo Bumbuli halina nia ya kusema kwamba COD ndio suluhisho pekee la tatizo la maendeleo ya elimu au ufumbuzi wa matatizo yote katika mfumo wa elimu nchini lakini tunaamini inaonesha matarajio ya kutosha kuona thamani ya kujaribu, kujifunza na kutathmini.
Uendelevu wa program
Ili program iwe endelevu, Shirika la Maendeleo Bumbuli(BDC) litaweka mfumo thabiti wa kufanya tathimini na kutoa mrejesho, ambao utatumika kama zana ya kupimia uwajibikaji, na kuendeleza uwazi. Pia ni muhimu kuzingatia ushirikishwaji wa wenyeji wa Bumbuli na umiliki wa program ya COD. Hili linaweza kufanikiwa kwa kuanzisha kampeni ya kuhamasisha elimu bora kama uwekezaji wa wenyeji, na Mtandao wa Wahitimu wa Shule za Sekondari Bumbuli kwa ajili ya fedha za COD. Zaidi sana, Shirika la Maendeleo Bumbuli litahusisha na kutumia Bodi za Shule, ambazo zinahusisha wazazi na walimu. Hii ndiyo njia itakayowafanya watu wa Bumbuli wathamini juhudi zao wenyewe katika kuboresha jamii zao.
5. Kambi ya Wanafunzi Wanaojiandaa na Mtihani wa Kidato cha Nne 2012
Kuanzia tarehe 4 Agosti hadi 5 Septemba, wakati wa likizo za masomo, Shirika limeandaa kambi maalum kwa matayarisho ya vijana wanaojiandaa na mtihani wa Kidato cha Nne mwaka huu. Kambi hii itakuwepo kwenye Kituo cha Elimu Soni, ambacho kina mandhari, mazingira na eneo la kutosha kufundishia na kuishi wanafunzi katika kipindi hiki.
Kila siku, wanafunzi hao watapigwa msasa kwa masomo ambayo hawakupata fursa ya kuyasoma vizuri katika mwaka wa shule, watafundishwa mbinu za kufanya mitihani (ikiwemo time-management), na kufanya revision ya mitihani ya Kidato cha Nne ya kuanzia mwaka 1984 hadi sasa. Shirika litatafuta walimu wenye sifa za kufundisha masomo ya Hesabu, Kiingereza, Historia, Kemia, Fizikia na Biolojia, hata nje ya Jimboni na kuwalipa posho kuja kufundisha kwenye kambi. Pia tutaomba watu mbalimbali, ikiwemo walimu wastaafu, wenye moyo wa kujitolea waje kufundisha kambi hii.
Mwisho
Hadi sasa Shirika la Maendeleo Bumbuli halijapata mfadhili au ufadhili kutoka kokote au kwa mtu yoyote. Miradi hii niliyoitaja ndio iko katika hatua za kupata ufadhili. Fedha ambazo zimetumika hadi sasa kuanzisha Shirika, kuweka ofisi, kuajiri watumishi wa muda na kufanya utafiti na kutengeneza maandiko ya miradi zimetokana na mkopo niliouchukua kama Mbunge, ikiwemo mkopo wa gari ambao sikuutumia kununua gari bali kuanzisha Shirika.
Napenda kutoa mwito kwa wana-Bumbuli wenzangu na Watanzania kwa ujumla kusaidia kuchangia maendeleo ya Jimbo la Bumbuli, hasa kwa miradi ambayo hatukuitafutia ufadhili kama huu wa COD na kambi. Kwa kuchangia unaweza kutumia namba ya M-PESA 0762088050. Kwa maelezo zaidi kuhusu Shirika la Maendeleo Bumbuli, tuma barua pepe: getinvolved@bumbuli.org au piga simu: +255 22 2129821/6 au tuma fax: +255 22 2129796
Katika miezi ijayo, BDC pia itatekeleza miradi ya kitaifa yenye manufaa kwa maendeleo na utawala bora kwa nchi yetu. Naamini nchi yetu itapiga hatua za maendeleo kwa kasi zaidi kama kila mmoja wetu, kwa nafasi na uwezo wake, atathubutu, lakini pia kama sote tutasaidiana katika kuchangiana na kupeana mawazo kuhusu shughuli za maendeleo.

January Makamba
Mbunge Bumbuli

No comments:

Post a Comment