NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 8, 2012

JK aitisha mkutano wa dharura CCM

HALMASHAURI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (Nec), inatarajiwa kukutana kwa dharura mjini Dodoma Februari 12 mwaka huu.Kikao hicho cha Nec kinakuja kipindi ambacho upepo wa kisiasa ndani ya  chama hicho tawala umekuwa ukivuma vibaya, kufuatia wabunge wake kuingia katika vita ya chini chini na Serikali yao inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete.

Taarifa zilizopaatikana jana kutoka ndani ya CCM, zilisema tayari wajumbe wa Nec wamekwishafahamishwa kuwapo kwa kikao hicho cha dharura.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, pamoja na mambo mengine, kikao hicho cha Nec kitajadili masuala ya mchakato wa Katiba ya chama hicho.

Taarifa hizo zilifafanua zaidi kwamba, wajumbe watajadili jinsi ya kuwapata wajumbe wa Nec upande wa Zanzibar, baada ya katiba ya chama hicho kufanyiwa marekebisho kuhusu taratibu za kuwapata wajumbe hao.

Kauli Nape

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye  alithibitisha kuwapo kwa kikao hicho cha Nec na vingine vya chama hicho tawala lakini, akisema si vya dharura.

Nape alisema leo kutakuwa na kikao cha Sekretarieti ya chama hicho itakayokutana mjini Dodoma.
Kamati ya Maadili

Alitoa ratiba ya vikao hivyo akisema, Februari ya 11 mwaka huu kutakuwa na kikao cha Kamati ya Maadili asubuhi na kufuatiwa na kikao cha Kamati Kuu (CC) baadaye mchana.

Katibu huyo aliongeza kwamba, Febrauri 12 kutakuwa na kikao cha Nec huku ajenda kuu ikiwa ni kupitia mabadiliko ya katiba ya chama ili kuwezesha kufanyika kwa uchaguzi.

"Tunafanya hivyo kwakuwa kuna watu walikuwa wanahoji uchaguzi
utafanyikaje wakati Nec haijakaa, kwa hiyo hiki ni kikao maalumu cha mabadiliko ya katiba ili uchaguzi ufanyike, " alisema Nape.

CCM imeanza mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa ndani ya chama hicho ambao uchukuaji wake wa fomu ulianza Februari 4 mwaka huu huku uchaguzi ukitarajiwa kuendelea awamu kwa awamu, kuanzia jumuiya na chama hadi Juni.

Vikao hivyo vya juu vya chama vinafanyika wakati pia chama hicho kikiwa bado hakijatekeleza mpango wa kujivua gamba ambao kwa sasa ulirudishwa CC kwa ajili ya maamuzi ya mwisho.


JK alivyowalainisha

Hata hivyo, juzi Rais  Kikwete alifanikiwa kuwalainisha wabunge hao wa CCM, ambao walikuwa wameweka msimamo wa kukataa Muswada wa Marekebisho ya Mabadiliko ya Katiba.

Katika kikao hicho kilichohudhuriwa na wabunge wachache, walikubali kupitisha muswada huo ambao unatarajiwa kuwasilishwa bungeni leo.

Baadhi ya wabunge waliohudhuria kikao hicho ni Jenister Mhagama (Peramiho), Peter Selukamba (Kigoma Mjini), Angela Kairuki (Viti Maalumu), Anna Kiliango (Same Mashariki), Saidi Nkumba (Sikonge), Christopher Ole Sendeka (Simanjiro) na Muhammad Amour Chomboh (Magomeni).

Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho, wabunge hao walifikia uamuzi huo baada ya Rais Kikwete kuwaeleza kwamba bado wanayo nafasi ya kufanya marekebisho wanayoona yanafaa, kwa sababu yaliyopelekwa na Serikali ni mapendekezo.

“Kwa kweli tumemwelewa Rais, mwanzo kuna vitu ambavyo vilikuwa hatujaelezwa vizuri. Rais alichotwambia ni kwamba sisi ndiyo waamuzi wa mwisho, Serikali imeleta mapendekezo tuna haki ya kufanya marekebisho kwa sababu hiyo ndiyo kazi yetu,” alisema mmoja wa wabunge hao na kuongeza:

“Rais ametwambia hakuwa na makosa kukutana na Chadema, amekutana nao kama alivyofanya kwa makundi mengine, na mapendekezo yao amatuletea sisi ndiyo waamuzi tupime wenyewe.”

No comments:

Post a Comment