NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 1, 2012

Mwenyekiti CCM ampa kipigo katibu wake

HALI ya kisiasa ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) katika wilaya ya Maswa, mkoa wa Shinyanga, si shwari kutokana na mwenyekiti wa chama hicho wilayani humo, Peter Bunyongoli, kumpatia kipigo katibu wake, Omari Kilolo, baada ya kutofautiana katika kikao cha kamati ya siasa.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya kikao hicho na kuthibitishwa na baadhi ya wajumbe kilichofanyika katika ofisi ya katibu wa CCM wilaya  iliyoko mjini humo  zinaeleza kuwa tukio hilo lilitokea Jumatano iliyopita, majira ya saa 7:30 mchana.
Wajumbe hao wakizungumza na waandishi wa habari mjini Maswa jana kwa masharti ya kutotajwa majina, walieleza chanzo cha katibu huyo kupata kipigo ni hoja iliyokuwa ikijadiliwa ya matumizi ya fedha sh milioni 26 zilizotokana na malipo ya mnara wa simu za mikononi wa kampuni ya Vodacom ulioko juu ya jengo la ghorofa moja la ofisi hiyo.
Viongozi hao waliendelea kushutumiana juu ya matumizi mabaya ya fedha hizo huku kila mmoja akimtupia lawama mwenzake, jambo ambalo lilizua mtafaruku mkubwa ndani ya kikao hicho.
“Wakati tukiendelea na hoja hiyo viongozi hao kila mmoja alianza kumtupia lawama  mwenzake juu ya matumizi mabaya ya fedha hizo ambazo zilianza kutumika tangu katika kampeni za uchanguzi mkuu uliopita,” alisema mjumbe mwingine.
Habari zaidi zinazidi kueleza kuwa katibu huyo aliendelea kumtupia lawama mwenyekiti wake kwa kushindwa kukisimamia chama tangu aliposhindwa ubunge wa jimbo la Maswa Mashariki na Mbunge wa sasa Sylvester Kasulumbayi (CHADEMA), hivyo kukitelekeza hadi alipoibukia katika kikao cha kamati ya siasa na kumtupia lawama juu ya matumizi ya fedha za mnara.
Kauli hiyo ndiyo iliyompandisha hasira mwenyekiti huyo na kusimama na kuanza kumshambulia kwa kumpiga ngumi, jambo ambalo liliwashangaza wajumbe na ndipo Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Kapteni James Yamungu alipotaka busara itumike katika kufikia muafaka jambo hilo.
“Akizungumzia tukio hilo, katibu wa CCM wilaya ya Maswa, Omari Kalolo, alikiri kupata kipigo kutoka kwa mwenyekiti wake na kusisitiza kuwa kitendo alichokifanya hakipaswi kufanywa na kiongozi.
“Ni kweli mwenyekiti wangu amenipiga ngumi tukiwa ndani ya kikao cha kamati ya siasa, nimesikitika sana,  kwani jambo hili si siri kwani kwa sasa kila mtu analifahamu na kitendo alichokifanya hakikupaswa kufanywa na kiongozi aliyepewa dhamana ya kusimamia ilani ya chama chenye kuongoza dola,” alisema.
Alipotafutwa kwa njia ya simu mwenyekiti wa CCM wilaya ya Maswa, Peter Bunyongoli, kuzungumzia tukio hilo simu yake ya mkononi ilikuwa ikiita mara kwa mara bila kupokelewa.

No comments:

Post a Comment