NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 1, 2012

Wanajeshi waanza kazi Muhimbili

MADAKTARI wanajeshi 15, kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), jana walianza  kutoa huduma za kitabibu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Madaktari hao walipelekwa katika Idara ya Magonjwa ya Dharura huku Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Haji Mponda akiahidi kuongeza wengine 80 kutoka wizarani kwake.
Mwandishi wetu alitembelea baadhi ya wodi katika hospitali hiyo na kuona wagonjwa wasiozidi 10, ilhali wodi hizo zinachukua kati ya wagonjwa 80 hadi 90.
Mmoja wa wagonjwa aliyelazwa katika jengo la Kibasila, wodi namba 14, ambaye hakupenda kutaja jina lake, alisema  jana asubuhi daktari mmoja alipita na kumchoma sindano.
Katika Jengo la Kibasila, wodi namba 12, msimamizi wa wodi hiyo, bila kujua kuwa alikuwepo mwandishi wa habari hizi, alisikika akimwambia mfanyakazi mwingine wa hospitali hiyo, wauguzi tokea juzi hawapo wodini kwa kuwa wako kwenye mkutano wao unaoendelea.
Awali akizungumza na waandishi wa habari, ofisa habari wa hospitali hiyo, Aminaeli Eligaesha, alisema juzi katika eneo hilo la Idara ya Magonjwa ya Dharura, ambako wamewekwa madaktari hao wa JWTZ, wagonjwa hawakupokelewa kutokana na mgomo uliopo.
Alibainisha kuwa mkuu wa idara hiyo, Profesa Victor Mwafongo, aliamua kuomba msaada na ombi hilo liliitikiwa vema kwa madaktari  wa JWTZ kupelekwa hospitalini hapo jana.
“JWTZ wametupatia madaktari 15, wameripoti leo (jana) saa mbili asubuhi, sasa hivi wanatembea kwa ajili ya kujifunza mambo mbalimbali,” alisema Aligaesha.
Alisema madaktari hao wanajeshi waliofika hospitalini hapo wote ni mabingwa kwa kuwa wako wenye fani ya upasuaji, magonjwa ya wanawake, watoto na meno.
Alitoa wito kwa Watanzania kuwapeleka wagonjwa hospitalini hapo, kwa kuwa hali hivi sasa imetengamaa na kwamba mambo mengine yanaendelea kurekebishwa.
Waziri wa Afya
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda, alifika hospitalini hapo, jana asubuhi kuangalia athari za mgomo huo uliodumu kwa takriban wiki mbili sasa.
Alisema baada ya hali ya hospitalini hapo kusuasua serikali imepeleka wanajeshi hao na pia wizara yake inatarajia kupeleka madaktari 80 ambao watatawanywa kwenye vitengo tofauti kuongeza nguvu kwa wachache waliopo.
Waziri huyo alisema mlango wa serikali wa kuzungumza na madaktari hao bado uko wazi, kwa kuwa kuna taratibu za kufuata kwa watumishi wa umma ili wazungumze na kufikia muafaka.
Wanaharakati wazungumza
Wanaharakati  hapa nchini wametoa wito kwa serikali na madaktari kurejea kwenye meza ya mazungumzo ili huduma za afya zitolewe kama ilivyokuwa kabla ya mgomo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Sikika, Irene Kiria, aliitaka serikali iache kulifanya suala hilo kuwa la kisiasa bali walipe uzito kwa sababu linagusa uhai wa wananchi wengi.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Helen Kijo-Bisimba, alihoji kauli aliyoitoa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuwa kama madaktari wasingerudi kazini, serikali ingetumia wanajeshi.
Dk. Kijo-Bisimba, alihoji kama hospitali za majeshi nchini zina madaktari wa kutosha kwa nini hawatoi huduma kwa watu wakati taifa lina upungufu wa madaktari kwa zaidi ya asilimia hamsini.
“Madaktari hao watakapoondolewa kwenye hospitali zao, je huduma katika hospitali hizo walizotoka zitakuaje?
“Je madaktari wa jeshi malipo yao yanatofautiana na madaktari wetu wa kawaida? Gharama za kuwapeleka kwenye hizo hospitali na kuwatunza hazitakuwa zimeongeza mzingo mwingine kwa taifa?” alihoji mkurugenzi huyo.

No comments:

Post a Comment