NJOMBE

NJOMBE

Friday, February 10, 2012

Waziri wa Afya Bado natathimini,Nitatoa maamuzi


Waziri wa Afya Dk Haji Mponda
WAKATI Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Blandina Nyoni na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa wakisimamishwa kazi, Waziri wa wizara hiyo, Dk Haji Mponda, amesema kukimbilia kujiuzulu kabla ya kutathimini jambo husika siyo suluhu ya kutatua tatizo.

Dk Mponda na Naibu wake, Dk Lucy Nkya, wamekuwa wakishinikizwa na madaktari pamoja na mawaziri wenzao, kuwajibika kwa kujiuzulu kutokana na mgomo huo wa zaidi ya wiki mbili uliotikisa nchi.Akizungumza jana na gazeti hili kwa njia ya simu lililotaka kujua msimamo wake, kama yuko tayari kuwajibika kutokana na mgomo huo, ama la Dk Mponda  alisema;

"Kukimbilia kujiuzulu siyo suluhu sana ya tatizo. Kwasababu kama ni hivyo, watu wanaweza kuharibu mambo kwa maksudi wakitegemea watajiuzulu na kukaa pembeni."

Alieleza kwamba hadi jana jioni,  hakuwa na uamuzi wowote kuhusu hilo na alikuwa akiendelea na majukumu yake kama kawaida huku akisisitiza;

"Unajua mtu anaweza kufikiria zaidi kujiuzulu  kama atakuwa amefanya au amesababisha kitu na yeye mwenyewe nafsi yake ikathibitisha hilo. "

Alisema binafsi, ameguswa na mgomo huo wa madaktari ambao umeathiri huduma za afya nchini, huku baadhi ya watu wakipata madhara zaidi ya maradhi.

Lakini, alipoulizwa kwamba kutokana na hali hiyo, haoni kwamba alipaswa kuwajibika kwa kujiuzulu kama sehemu ya kuumizwa na madhara yaliyowapata Watanzania kutokana na Wizara yake  alijibu; "Naomba ni reserve(nihifadhi) kauli yangu katika hilo. Lakini, nani wanataka nijiuzulu, ni wewe (mwandishi) au nani? Maana sijasikia hilo unalosema. Nikisikia nitaamua."   
 
Alifafanua kwamba kuwajibika wakati mwingine baadhi ya watu wamekuwa wakitafsiri dhana hiyo tofauti .

"Kwa mfano, mimi nimeguswa sana na mgomo wa madaktari, nawapenda sana Watanzania, sasa hapo kuna tofauti kidogo."

Dk Mponda alisema ndiyo maana alikuwa akifanya jitihada zote kuhakikisha anakutana na madaktari hao kuhakikisha mgomo huo unamalizika, lakini bahati mbaya juhudi hizo hazikufanikiwa haraka.

"Kwakweli nimeguswa sana na mgomo huo wa madaktari, ndiyo maana nimekuwa  nikifanya kila jitihada kuhakikisha unamalizika, lakini bahati mbaya hilo halikutokea. Kwa hiyo, nimeumia sana," alisisitiza  Dk Mponda, baada ya  kuulizwa tena kwamba kama ameguswa ni kwanini  asiwabijike kwa kujiuzulu hata kama hakutenda kosa.

Alisema anatambua umuhimu na dhana ya uwajibikaji, lakini akasisitiza kuwa "Siwezi kusema zaidi kwa sasa. Wakati ukifika nitaweza kuzungumza."


Mawaziri wenzake
Katika kikao cha kazi kilichofanyika Jumanne iliyopita chini ya Waziri Mkuu Pinda, ilidaiwa kutoka ndani ya kikao kwamba baadhi ya mawaziri  walimweleza mkuu huyo wa shughuli za Serikali bungeni kwamba, Waziri wa Afya na Naibu wake, walipaswa kujiuzulu.

Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho, zilidai kuwa suala la mgomo huo, lisingeweza kushughulikiwa kimyakimya, na kwamba ilikuwa lazima Serikali kukubali kukaa na madaktari hao na kusikiliza malalamiko yao.

Tayari, pendekezo hilo lilishatolewa na Kamati ya Wabunge wa CCM, ambao walitaka Dk Mponda, Naibu wake Dk Nkya na Katibu Mkuu Nyoni wajiuzulu na wakikataa wawajibishwe.

No comments:

Post a Comment