NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, February 1, 2012

Slaa akutana na JK

KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, amemtaka Rais Jakaya Kikwete kutoa tamko iwapo ameridhia wananchi waendelee kufa kwa kukosa huduma za afya kwa kukataa kuwaongezea posho madaktari huku akiidhinisha posho ya sh 330,000 kwa siku kwa wabunge.
Amesema Rais Kikwete amekuwa mgumu kuongeza posho kwa watu wanaotoa huduma muhimu kama madaktari na walimu, lakini amekuwa mwepesi kwa wanasiasa ambao hukaa kimya bungeni na wengine kuishi kupiga makofi.
Kauli hiyo aliitoa jana alipokuwa akizungumza na Tanzania Daima, kwa njia ya simu. Dk. Slaa alisema iwapo Rais Kikwete hatatoa tamko kuhusu suala hilo, CHADEMA itayatumia majukwaa kuwaeleza wananchi.
Alisema CHADEMA imekuwa ikilaumiwa kwa kuishtaki serikali kwa wananchi kila inaposhindwa kuwajibika lakini hivi sasa hawatakali wala kuogopa lawama hizo kwakuwa hazina msingi.
“Sasa imetosha. Rais Kikwete atoe tamko  kama ameidhinisha wananchi waendelee kufa kwa kugoma kupandisha posho ya sh 10,000 kwa madaktari na kuwaongezea wabunge.  Hivi anataka nchi iendelee hivi hadi lini?” alihoji.
Alisema kuwa madaktari wengi nchini wanafanya kazi katika mazingira magumu huku wakihatarisha maisha yao kutokana na kuwapo katika hatari ya kuambukizwa magonjwa, lakini serikali haiwajali kwa kiwango inachowajali wanasiasa.
Alibainisha kuwa serikali inapaswa kulaumiwa kwa hali inayoendelea sasa nchini kwa wananchi kufa kutokana na kukosa huduma za matibabu katika hospitali mbalimbali hapa nchini.
Aliongeza kuwa mgomo wa madaktari umeonyesha kuwa serikali imekosa umakini katika vipaumbele vyake na hivyo kuwafanya wananchi waishi maisha ya taabu kila kukicha.
“Rais Kikwete alipaswa kukaa chini na kuziongezea posho kada zote … sasa hakuna uwiano, jambo ambalo ni hatari kwa nchi. Mwaka 2007 niliwahi kusema bungeni kuwa kuna bomu litalipuka, Pinda (Waziri Mkuu, Mizengo Pinda) alikataa,” alisema.
Juzi, Waziri Mkuu alikaririwa akisema kuwa Rais Kikwete ameidhinisha ongezeko la posho za vikao (sitting allowance) kwa wabunge kutoka sh 70,000 hadi sh 200,000 kwa siku.
Kuidhinishwa kwa posho hiyo kunafanya sasa mbunge kupokea sh 330,000 kwa siku. Sh 200,000 ikiwa ni posho ya kikao, sh 80,000 posho ya kujikimu na sh 50,000 nauli.
Pinda  alitoa taarifa hiyo katika kikao cha utangulizi cha wabunge ambako inaelezwa kuwa mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), na mbunge wa Bumbuli, January Makamba (CCM) walipinga suala hilo.
Mjadala wa kupanda kwa posho hizo umeligawa taifa tangu kuibuliwa kwake huku baadhi ya makundi yakipinga ongezeko hilo.
Jana Spika wa Bunge, Anna Makinda, alisema posho hizo mpya zimeanza kulipwa kuanzia jana baada ya kupitishwa na ngazi zinazohusika.

No comments:

Post a Comment