NJOMBE

NJOMBE

Tuesday, January 24, 2012

Mengi awalipua wapambanaji ufisadi

  Awatuhumu kuhongwa, akerwa na mbio za urais

MWENYEKITI wa kampuni za IPP, Reginald Mengi, amesema anakerwa na wapambanaji wa ufisadi kunyamaza kimya kwa kile alichokiita kuhongwa na mafisadi au wameanzisha mikakati inayolenga kuzorotesha nguvu ya vita dhidi ya ufisadi.
Licha ya Mengi kutowataja wapambanaji hao, kauli hiyo inaelekea kuwalenga baadhi ya wanasiasa ambao walijimbapambua kuwa ni wapambanaji wa ufisadi hasa katika Bunge la tisa lililokuwa chini ya Spika wake Samuel Sitta.
Katika Bunge hilo wabunge waliojipambanua kuwa ni wapambanaji wa ufisadi ni Dk. Harrison Mwakyembe (Kyela), Anne Kilango Malecela (Same Mashariki), James Lambeli (Kahama), Lucas Selelii (Nzega), Beatrice Shelukindo (Kilindi) na Christopher Ole Sendeka (Simanjiro).
Mengi alitoa kauli hiyo juzi katika ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam kwenye tafrija ya chakula cha mchana kilichoandaliwa na IPP kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Alisema katika siku za hivi karibuni wapambanaji wa ufisadi, ikiwa ni pamoja na vyombo vya habari, wamenyamazishwa kwa njia mbalimbali kutokana na nguvu za mafisadi kifedha.
Alisema ingawa vitendo vya ufisadi vimeongezeka kwa nguvu na kasi kubwa, nguvu na kasi ya wananchi kwa kushirikiana na vyombo vya habari katika vita hiyo zimepungua ambapo hivi sasa kelele za kulaani ufisadi hazisikiki kama awali.
“Kuna watu wanaofikiri kwamba kupungua kwa kelele hizo kunaashiria kupungua au kutokomea kwa ufisadi, kumbe si kweli bali ni kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo ya rushwa ya fedha za mafisadi,” alisema.
Alitaja sababu nyingine kuwa ni kutochukuliwa kwa hatua kwa watu wanaohusishwa na vitendo vya ufisadi ambao wanajulikana kwa majina lakini wameachwa wakiendelea kula maisha ya raha na yenye jeuri.
“Ripoti nyingi za uchunguzi uliofanywa na vyombo vya habari zimefichua ufisadi mkubwa wa aina mbalimbali ambao haukupata kukanushwa, kwa mfano Kagoda na Meremeta, ikiwa na maana kwamba ripoti hizo ni za kweli. Ripoti hizi ni za muda mrefu sana, lakini hadi sasa waliohusishwa na ufisadi huo hawajachukuliwa hatua.
“Wananchi wanashangaa kuona mchota fedha za EPA anakiri uporaji huo na anatamba amerudisha fedha, lakini hachukuliwi hatua yoyote, eti kwa sababu hakuna ushahidi. Kama kurudisha si ushahidi, ni ushahidi wa aina gani unatakiwa?” alihoji.
Alisema wananchi wanashangaa wanapoona wauzaji wa rada iliyonunuliwa kwa bei ya kulangua wanarejesha nchini fedha walizoongeza katika uuzaji huo lakini serikali ya Tanzania haijawachukulia hatua zozote za kisheria waliofanikisha rada hiyo kununuliwa kwa bei ghali.
Mengi alisema mfumo mzima wa jamii umechafuliwa na ufisadi unaohusisha viongozi wa serikali, wanasiasa na baadhi ya vyombo vya habari katika vitendo vya rushwa na viongozi wa umma katika wizi na uporaji wa mali za umma.
Aliongeza kuwa kutokana na kutochukuliwa hatua za kisheria dhidi ya wale wanaohusishwa na ufisadi na uchafuzi uliosababishwa na ufisadi katika mfumo wa jamii, wananchi wamekata tamaa ya ushindi katika mapambano dhidi ya ufisadi.
Alionya kuwa ufisadi unavunja amani na ni mchezo hatari na wa mauti, hivyo ni lazima vitendo vya ufisadi vichukuliwe hatua za kisheria haraka vinapobainika.
Pamoja na hayo, alieleza kuwa mapambano dhidi ya ufisadi ni lazima yawe endelevu na kwamba dhamira ya kutokomeza ufisadi huo bado wanayo ingawa mapambano ya awali yalizaa matunda yasiyoridhisha.
“Mafanikio haya yawe chachu ya kuongeza nguvu katika mapambano na tusikubali kukata tamaa kutokana na kutoridhishwa na kiwango cha hatua zilizochukuliwa. Kukata tamaa ni kukubali kushindwa. Bado hatujashindwa.
“Tusikubali kurubuniwa na nguvu ya kifedha za mafisadi, tusikubali kunyamazishwa. Tukikaa kimya tumewasaidia mafisadi na kuwasaliti ndugu zetu walalahoi.
Mbio za urais
Alisema mbio za kutaka kuwania urais hasa kupitia chama tawala (CCM), zimefikia hatua mbaya kutokana na baadhi ya wanasiasa na watendaji kusahau kuwatumikia wananchi.
Alisema baadhi ya viongozi wa umma wenye dhamana ya kushughulikia matatizo ya wananchi wameyapa kisogo matatizo hayo na badala yake kushughulikia mambo yao binafsi, kiasiasa na kiuchumi.
“Badala ya kushindana katika kuwasaidia wananchi wanashindana katika kujitajirisha na kutafuta madaraka ya kisiasa kuelekea mwaka 2015,” alisema Mengi.
Alisema sababu hiyo na nyinginezo zinachangia maisha ya wananchi kuwa magumu na kubainisha kuwa zipo sababu ambazo haziepukiki, lakini zipo ambazo zinaweza kuepukika.
Katika hatua nyingine, mwenyekiti huyo aliwashukia watendaji wa halmashauri wa miji na wilaya kwa ubadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo.
Alisema miradi mingi ya maendeleo haitekelezwi na hata kama ikitekelezwa inakuwa ya kiwango cha chini na kwa gharama kubwa na kusababisha hasara kubwa, jambo ambao linaashiria kuwapo kwa rushwa katika utoaji wa zabuni.
“Halmashauri za miji na za wilaya ni kitovu cha maendeo ya jamii, lakini maendeleo katika halmashauri nyingi yamekuwa hafifu na ushahidi umeonyesha kwamba baadhi ya viongozi wa umma katika halmashauri hizo wamekuwa wabadhirifu, waporaji na wezi wa fedha za maendeleo,” alisema.
na Tamali Vullu

No comments:

Post a Comment