NJOMBE

NJOMBE

Monday, January 23, 2012

Raia wa Nigeria anaswa na dawa za kulevya Dar

RAIA wa Nigeria mwenye miaka 34 amekamatwa na polisi wa Uwanja wa Ndege Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere akiwa na dawa za kulevya tayari kuelekea nchini Nairobi.

Kukamatwa kwa Mnigeria  huyo  kumekuja siku chache baada ya polisi kukamata kiasi kikubwa cha dawa za kulevya zipatazo kilo 210 mkoani Lindi, ambazo zilikuwa tayari kusafirishwa kwenda jijini Dar es Salaam zikivunja rekodi tangu kuanzishwa kwa Kitengo cha Dawa za Kulevya.

Juzi, Polisi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere walimkamata Mnigeria huyo jambo ambalo lilithibitishwa na  Kamanda wa Polisi wa Viwanja vya Ndege nchini, Ulrich Matei akisema lilitokea  saa 10:20 alfajiri.

Matei alisema kutokana na kuimarishwa kwa shughuli za upekuzi uwanjani hapo, waliweza kumbaini raia huyo akiwa na pipi 14 za dawa za kulevya ambazo zinaendelea kuchunguzwa kujua ni za aina gani.

Alifafanua kwamba, mtuhumiwa huyo mwenye hati ya kusafiria namba A02425579 iliyotolewa Nigeria mwaka 2010, alikuwa akijiandaa kuondoka na ndege ya Shirika la Ndege la Kenya (KQ).

Kamanda Matei aliongeza, baada ya kupekuliwa raia huyo alikutwa na kiasi hicho ambacho alikificha kwenye fulana na kuongeza kwamba alikuwa akisafiri na ndege hiyo kwenda Kenya kisha Lagos, Nigeria.

"Hapa uwanjani tunajitahidi kwa uwezo wetu wote kuhakikisha uwanja wetu hauwi njia ya wahalifu. Hatuwezi kuruhusu watu wachafue taswira nzuri ya nchi yetu. Sasa tulivyompekua, tulimkuta akiwa na kiasi hicho cha pipi akiwa amezifunga kwenye fulana.

 Alikuwa anasafiri na ndege ya Shirika la Ndege la Kenya yenye namba KQ481 akielekea Nairobi kisha Lagos, Nigeria," alifafanua Kamanda Matei.

Hata hivyo, Matei alisema raia huyo bado alikuwa akishukiwa kuwa na dawa nyingine alizomeza tumboni lakini hadi jana hakuwa ameweza kutoa nyingine na alikabidhiwa kwenye kikosi cha Kudhibiti za Dawa za Kulevya kwa taratibu zaidi za kisheria.

"Tulimshuku alikuwa amemeza dawa tumboni lakini hadi jana asubuhi hakuwa ameweza kutoa. Tulichofanya sisi Polisi wa Uwanja wa ndege ni kumkabidhi Kitengo cha Dawa za Kulevya ili waweze kuendelea na taratibu nyingine ikiwa ni pamoja na kumpiga X-ray na vipimo vingine kubaini aina ya dawa hizo alizokamatwa nazo kwani zinahitaji vipimo," alifafanua kamanda Matei.

Alisema licha ya kumshikilia kwa siku nzima ya juzi raia huyo ambaye alikamatwa Terminal Two, hakuweza kutoa dawa nyingine zaidi na kwamba  taratibu nyingine za kisheria zitaandaliwa.

No comments:

Post a Comment