NJOMBE

NJOMBE

Tuesday, January 24, 2012

Ofisa Bodi ya Mikopo adaiwa kuiba mil. 90/-Aghushi majina hewa ya wanafunzi

MFANYAKAZI wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HELSB), Ester Budili, amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, akikabiliwa na tuhuma tisa za kughushi majina hewa ya wanafunzi na kisha kujipatia sh zaidi ya sh milioni 90.7 kwa udanganyifu.
Akisomewa mashtaka yake jana mbele ya Hakimu Mkazi Binfi Mashabala, Wakili wa Serikali, Frida Mwale, alidai kuwa kati ya Agosti 5 mwaka 2010 na Aprili 24 mwaka jana katika ofisi ya Bodi ya Mikopo, iliyoko Msasani, alighushi majina ya wanafunzi na kuyaingiza kwenye orodha ya majina ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Bugando kuwa ni miongoni mwa wanafunzi wanaoomba mikopo.
Mwale aliyataja majina ya wanafunzi hao hewa kuwa ni John Suzane, Peter Bahati Mombo Yusuf, Bitaliho Gordian, Kwangaya Ibrahim, Majaliwa Nandu, Mtitu Catherine, Happy Alfred, Simon Isack na Julian Nyangige.
Alidai kuwa katika shtaka la pili anadaiwa kuwa katika kipindi hichohicho alighushi majina mengine ya wanafunzi hewa ambayo ni Catherine Nkya, John Nkya, Andrew John, Goliama Ally, Simon Pamela, Gash Damian na Suzane John na kuyaingiza kwenye orodha ya majina ya wanafunzi wa Chuo cha Uhandisi na Teknolojia (CoET) na kuonyesha kuwa ni miongoni mwa wanafunzi wanaomba mikopo kwa ajili ya elimu ya juu, huku akifahamu jambo hilo si la kweli.
Wakili Mwale aliendelea kudai kuwa katika shtaka la tatu, mtuhumiwa anadaiwa kughushi majina hewa ya wanafunzi Suzane John, Mella Christopher, Zake Ezra, Goliama Ally, Simon Michael, Peter Massawe, Naruo Peter, Pamela Simon na Catherine Nkya na kuwaingiza kwenye orodha ya wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo na Ustawi wa Jamii wanaoomba mikopo.
Aidha, alidai katika kipindi hicho alighushi majina ya wanafunzi Pamela Simon, Munisi Grace na Hamza Goliama kwamba ni wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wanaostahili kupewa mikopo ya elimu ya juu.
Alidai kuwa pia alighushi majina hewa ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Uuguzi cha Kilimanjaro kinachomilikiwa na taasisi ya kidini ya Kikristo, Chuo Kikuu cha Mzumbe, Tumaini,Chuo cha Makumila na Ruaha na kwamba wanafunzi hao walikuwa wanastahili kupewa mikopo na bodi hiyo.
Katika shtaka la kumi, wakili wa serikali alidai kuwa katika kipindi hicho mtuhumiwa aliiba sh milioni 90.7, mali ya bodi hiyo.
Hata hivyo, mtuhumiwa alikana tuhuma hizo na yuko nje kwa dhamana ya bondi ya sh milioni 45. Kesi imeahirishwa hadi Februari 7 itakapotajwa tena.
Habari na Happiness Katabazi

No comments:

Post a Comment