NJOMBE

NJOMBE

Monday, January 23, 2012

Arumeru waupokea mwili wa Mbunge kuuzika leo

MAMIA ya wakazi wa wilayani Arumeru na Jiji la Arusha, jana walijitokeza barabara kuupokea mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, Jeremiah Sumari ambaye atazikwa leo katika  eneo la Akeri wilayani Arumeru.


Mwili wa mbunge huyo, ambaye alifariki akiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Januari 17, mwaka huu, uliwasili jana majira ya saa 12:30 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwa ndege ya kampuni ya 540 ukisindikizwa na wabunge na mawaziri kadhaa.


Baadhi ya mawaziri waliowasili uwanjani hapo na ndege nyingine ya kusindikiza   mwili huo ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (mahusiano) Steven Wassira, Waziri wa Habari,Vijana ,Utamaduni na Michezo, John Nchimbi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera na Bunge), William Lukuvi.


Pia alikuwapo Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa ambaye alikuwa kwenye ndege moja na mwili wa Sumari na uwanjani hapo walikuwapo Manaibu Mawaziri kadhaa, akiwamo Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Godluck Medeye ambaye ni mbunge Jimbo la Arumeru Magharibi.


Magari zaidi ya 50 yaliyokuwa na watu mbalimbali wakiwamo mawaziri, wabunge na viongozi wa vyama vya siasa hususan  CCM yalionekana na kuvuta hisia za huzuni kwa wakazi wa mitaa mbalimbali yalikopita.
Wengine ni pamoja na viongozi wa Jumuiya ya Vijana ambao waliongozwa na Makamu Mwenyekiti wa( UVCCM), Beno Malisa na Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha, James Millya.

Akizungumza nyumbani kwa marehemu Sumari, Msemaji wa Familia ya Sumari, Chifu Esrom Sumari alisema wamepokea msiba huo kwa  masikitiko makubwa.


Chifu Sumaru ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa ukoo za Kabila la Wameru alilishukuru Bunge kwa kugharamia usafiri na mazishi ya Sumari na pia Serikali kwa kujitolea kumtibu Sumari nchini India na alipokuwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Chifu Sumari alisema kifo cha Mbunge huyo ni pigo kubwa kwa familia yao, kwani alikuwa mshauri muhimu na alitoa msaada mkubwa kwa familia na wakazi wa Jimbo la Arumeru Mashariki.


Hadi jana jioni, kamati ya mazishi ya mbunge huyo, ilikuwa inakutana ambapo ratiba ya awali iliyotolewa ilieleza shughuli za mazishi zitaanza saa 2:00  asubuhi.

Ratiba hiyo, inaeleza kuwa ibada ya mazishi itaanza saa 7:00 mchana katika Kanisa la Kiijili la Kilutheri Tanzania (KKKT) lilipo jirani na nyumbani kwa Sumari ambapo pia uwanja maalumu umeandaliwa kwa shughuli hiyo.


Viongozi mbalimbali wanatarajiwa kuhudhuria mazishi leo, akiwamo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye tayari yupo mjini hapa na kulikuwa na taarifa za Rais Jakaya Kikwete pia kuhudhuria mazishi hayo.

Marehemu Sumari ameacha mke na watoto wanne, na alichaguliwa kuwa mbunge tangu mwaka 2000 ambapo pia aliwahi kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi.



No comments:

Post a Comment