NJOMBE

NJOMBE

Thursday, January 26, 2012

Tanesco, Dowans waendelea kuvutana mahakamani

James Magai
MVUTANO mkali baina ya Shirika  la Umeme  Tanzania (Tanesco) na Kampuni ya Dowans, kuhusu hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu  ya Tanzania iliyoamuru Tanesco iilipe Dowans zaidi ya Sh 94 bilioni, bado unaendelea.

Mvutano huo unafautia hatua ya Tanesco kutafuta njia za kisheria baada ya kuomba kibali cha kukata rufaa katika Mahakama ya Rufani kupinga hukumu na  kuepukana na malipo hayo, lakini Dowans nayo ikaendelea kuibana kwa kuiwekea pingamizi ili inyimwe kibali hicho.

Septemba 28  mwaka jana, Jaji Emilian Mushi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, aliamua tuzo ya Dowans iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara (ICC), isajiliwe ili kuwa hukumu halali ya mahakama hiyo.

Kwa uamuzi huo, Tanesco sasa inatakiwa iilipe Dowans Sh 111 bilioni badala ya Sh 94 bilioni za awali.

Tanesco inapaswa kulipa fidia hiyo pamoja na riba ya asilimia 7.5.

Hata hivyo shirika hilo la umeme limeeleea kutokuridhishwa na hukumu hiyo na hivyo kutoa taarifa ya kusudio la kukata rufaa.

Maombi ya kutaka kibali cha kukata rufaa hiyo, yalitarajiwa kuanza kusikilizwa jana na Jaji Dk. Fauz Twaib lakini mahakama ilishindwa kuyasikiliza baada ya Dowans kuweka pingamizi, ikiomba mahakama isiipe Tanesco kibali.

 Dowans iliiwekea Tanesco pingamizi hilo mwezi huu ikidai kuwa kwa mujibu wa mkataba baina ya pande hizo, hukumu ya ICC haiwezi kukatiwa rufaa.

Ni hoja kama hizo ilizozitoa Dowansa wakati wa pingamizi la Tanesco kutaka Mahakama Kuu isiisajili tuzo yake na baadaye Jaji Mushi alikubaliana na hoja za Dowans na kuamuru tuzo hiyo isajiliwe.

Jana Jaji Dk Twaib aliziambia pande hizo mbili kuwa mahakama haitaweza kusikiliza maombi ya Tanesco kuhusu kibali cha kukata rufaa hadi hapo pingamizi la Dowans litakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.

Jaji huyo, alizitaka pande hizo, kuwasilisha hoja zao kwa njia ya maandishi na kwamba pingamizi hilo litaamuliwa Februari 16 mwaka huu, baada ya kupitia hoja zote.

Ikiwa mahakama itatupilia mbali pingamizi la Dowans, basi Tanesco itapewa kibali cha kukata rufaa kupinga hukumu hiyo.

Lakini kama mahakama itakubaliana na pingamizi la Dowans basi harakati za Tanesco kujinusuru katika malipo hayo kwa njia za kisheria zitakuwa mashakani.

Hukumu ya Jaji Mushi ilionekana dhahiri kwenda sambamba na kile alichowahi kukisema Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Fredrick Werema kuwa hakuna uwezekano wowote wa kisheria kuepuka malipo hayo.

Wakili wa Dowans, Kennedy Fungamtama  alisema hadi wakati hukumu hiyo inatoka, Tanesco ilipaswa kuilipa Dowans kiasi cha Sh 111bilioni badala ya Sh94 bilioni.

 “Fidia ya awali katika uamuzi wa ICC ilikuwa ni Dola za Marekani 65milioni, lakini kwa sasa ukiweka na riba ya asilimia 7.5 fidia hiyo imeongezeka hadi takribani Dola za Marekani 72milioni ambazo ni kama Sh111bilioni,” alisema Fungamtama.

Katika hukumu yake Jaji Mushi alisema baada ya kupitia mwenendo na hoja za pande zote nimebaini kwamba si sawa kwa mahakama hiyo kuingilia uamuzi wa ICC.

“Hivyo ninaagiza kuwa tuzo hiyo isajiliwe na iwe huku halali ya mahakama hii,” alisema Jaji Emiliani Mushi ambaye kabla ya kusoma hukumu hiyo alisema kuwa anatambua kuwa suala hilo limekuwa na msukumo mkubwa wa kisiasa lakini akabainisha kuwa anafanya kazi kwa mujibu wa sheria.

No comments:

Post a Comment