NJOMBE

NJOMBE

Monday, January 23, 2012

Lembeli, Mgeja wageuka kama wanamasumbwi


MBUNGE wa Kahama, James Lembeli, ambaye ametangaza kuwania nafasi ya uenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, amemtuhumu Mwenyekiti wa sasa, Hamisi Mgeja, kuwa ana ugonjwa wa kusahau.

Kauli hiyo imekuja baada ya Mgeja kudai kuwa, Lembeli hamnyimi usingizi na kumfananisha na sisimizi ambaye hawezi kumwathiri kwa sababu hana uwezo wa kushinda nafasi hiyo.

Lembeli alisema Mgeja siyo saizi yake katika nafasi yoyote ya kuchaguliwa na kwamba, hata yeye (Mgeja) anajua hasa kupitia uchaguzi mbalimbali uliopita ndani ya chama.

Alisema tayari amesahau mwaka 2005 alikuwa mgombea ubunge wa Kahama na kushindwa vibaya kura za maoni, alishika nafasi ya tatu kwa kupata kura 170 na kuongeza kuwa, hicho ni kielelezo tosha.
Mbunge huyo alisema Mgeja kwa kusahau, mwaka 2010 aligombea ubunge wa Kahama baada ya kukatwa Jimbo la Ushetu, lakini lilipofutwa hilo jipya alimkimbia kwa kujitoa.

“Mgeja siyo saizi yangu, alinikimbia uchaguzi wa kura za maoni za chama kwa mwaka 2005 na mwaka 2010, nilimshinda vibaya sasa hapo ndipo unapombaini kuwa anasahau,” alisema Lembeli.
Kuhusu kanuni ya CCM inayotaka mbungeau mtumishi wa Serikali kujiuzulu kwanza kabla ya kuwania wadhifa ndani ya chama, Lembeli alisema chama kinatoa vibali maalumu kwa wagombea wenye nafasi nyingine za uwakilishi, hivyo atafuata taratibu hizo mpaka amng’oe Mgeja.

Kwa upande wake, Mgeja alisema alimtaka mbunge huyo kuachana kumfuatafuata kwa sababu ana siri nyingi zinazomhusu, ikiwamo kujikita kupambana na ufisadi huku akitekeleza wapiga kura wake.

Mgeja alisema Lembeli anataka kucheza ngoma asiyolingana nayo na kwamba, ndani ya chama hakuna ushindani isipokuwa kuna kupangana, ndiyo maana (Lembeli) akapangwa kuwania ubunge, lakini siyo kwamba alimshinda.

“Mimi sitaki malumbano na Lembeli namheshimu sana, lakini akizidi nitafumua yake yote ninayofahamu ninayo na nitayaripua, yeye kama anataka uenyekiti agombee tu, lakini masuala ya kuzungumzia kitambi changu hayamhusu naona kama vile analionea wivu tumbo langu,” alisema Mgeja.

Mwaka jana, Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Shinyanga, iliwaita Lembeli na Mgeja na kuwaonya vikali kuacha malumbano, huku Mgeja akitolewa nje ya kikao baada ya Lembeli kugoma kujieleza mbele yake.

No comments:

Post a Comment