NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, October 24, 2012

URAIS 2015: Wanawake kuvuruga mambo CCM


•  Migiro, Tibaijuka, Nagu watajwa

Mh.Mary Nagu
HARAKATI za urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) zimeingia katika hatua mpya baada ya kuvuja kwa taarifa za kuwapo mkakati wa kuwapa nafasi wanasiasa wanawake na kuwatosa wanaume kwa kile kinachodaiwa kuvunja makundi yenye uhasama.
Habari za ndani ya makundi makuu ya wataka urais ndani ya CCM, zimethibitisha kuwapo taharuki kubwa miongoni mwao baada ya taarifa za wanawake kupewa nafasi kubwa kuzidi kushika kasi siku zinavyozidi kwenda.
”Kuna mpango wa kuwatosa wanaume kwa nia ya kuwapa fursa wanawake ndani ya CCM ili baadae atakayepatikana, akishinda akasaidie kulinda maslahi ya wale wasio na uadui wa kudumu, lakini wana maslahi ya kudumu (permanent interests)," alieleza mtoa habari wetu.
Mh.Anna Tibaijuka

Habari zinaeleza kwamba, nguvu kubwa iliyotumika katika maeneo mbalimbali nchini katika chaguzi za ndani ya CCM ni moja ya mikakati ya maandalizi ya mpango huo wa kuwasimika wanawake.
Wataka urais wanaolengwa kuzimwa ni pamoja na Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa, Edward Lowassa, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Wanawake wanaotajwa kufanikisha mpango huu ni Dk. Mary Nagu, Prof. Anna Tibaijuka na Dk. Asha Migiro ambao wote watasukumwa na makundi yenye fedha nyingi ili angalao wawili kati yao waingie hatua ya mwisho.
”Ambao wanatajwa kutaka kuingizwa hatua za mwisho ni Migiro na Tibaijuka ili wapate nafasi ya kupigiwa kura na wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM ambao kwa kiasi kikubwa wameandaliwa kwenye chaguzi za CCM zinazoendelea kwa mikakati maalum na kwa nguvu kubwa ya fedha,” kilisema chanzo chetu.
Mh.Asha Rose Migiro

Uchaguzi unaoendelea ndani ya CCM kwenye nafasi mbalimbali, una umuhimu wa peke yake mwaka huu kutokana na ukweli kwamba ndio uchaguzi wa mwisho ambao utaonesha sura halisi ya kuwapata wagombea wa nafasi za udiwani, ubunge na urais kwa tiketi ya CCM mwaka 2015.
Tayari makundi yameshajipanga kwa kuanza kufitiniana, kuwekeana mizengwe na mengi yanayofanana na hayo ili mradi tu watu wao wapite kwenye chaguzi hizi za ndani ya chama ili iwe rahisi kupata mtu wa kulinda maslahi yao au kujihakikishia ulaji pindi mtu wao atakapopita.
Kutokana na nguvu ya CHADEMA na kile kinachoonekana kwa wana CCM wenye ushawishi mkubwa kuogopana kwa sababu mbalimbali, kuna mkakati wa kuwa na 'plan B' ya kusimamisha wanawake, mkakati kama uliotumika kumzima aliyekuwa Spika wa Bunge, Samwel Sitta.
Sitta alijikuta akitolewa nje ya ulingo baada ya majina ya wanawake pekee kupitishwa na Kamati Kuu ya CCM kuwania nafasi hiyo ya uspika.
Wakati akitetea kiti cha uspika, Sitta ambaye sasa ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, alikuwa mstari wa mbele katika kupinga ufisadi baada ya kutajwa ya kuwa aliendesha kampeni ya kumng'oa aliyekuwa waziri mkuu kwa wakati huo, Lowassa, kwa kulazimishwa na Bunge kujuzulu kutokana na kashfa ya kampuni tata ya kufufua umeme ya Richmond.
”Hapa Sitta alikuwa hana jinsi ila kusalimu amri, na yakafanyika yaliyokusudiwa na wabaya wake wanaounga mkono ufisadi.
“Hii plan B inaweza kutumika kabisa kwenye uchaguzi ujao 2015 kutokana na mikakati yenye hila inayohusisha fedha nyingi inayoendelea ndani ya CCM,” kilisema chanzo chetu.
Kwa kadri muda unavyokwenda, kumekuwa na ongezeko la malalamiko kwenye chaguzi za CCM katika ngazi mbalimbali kutokana na nguvu kubwa ya fedha kutumika kama njia ya kujipanga kwenye kupitisha jina la mgombea kwenye nafasi ya urais.
Mfumo ulioko sasa hivi wa kuwatumia wajumbe wa halmashauri kuu za wilaya/mikoa kuchagua wawakilishi wa kwenda kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) na Mkutano Mkuu wa Taifa umeonesha kuwa na dosari kubwa sana kutokana na rushwa kubwa ya fedha inayotumika kuwapata wawakilishi hawa.
Watu wenye malengo ya kugombea urais na wapambe wao wamekuwa wanatoa fedha nyingi kwa watu wanaowataka kwenye mikoa na wilaya ili pindi watakapochaguliwa wakawapigie kura ya kuwapitisha kwenye NEC na mkutano mkuu wa taifa.
"Kwa kweli rushwa za namna hii ni hatari sana na zinaweza kutupatia viongozi wa ajabu na wapenda rushwa kutokana na mbegu waliyoiotesha tokea kwenye msingi. Demokrasia nzuri ni ile ya kupanua wigo ili pawe na matokeo mazuri na yenye maslahi mapana zaidi," alisema mstaafu mmoja wa CCM.
Baadhi ya wastaafu na wana CCM wanaochukia rushwa wanapendekeza kuwapo kwa baraza rasmi la mwisho la kupitisha jina la mgombea wa urais hata kama amepitishwa na vikao vya NEC na mkutano mkuu.
"Pengine baraza hili liwe na marais wastaafu, makatibu wakuu wastaafu, watu wenye weledi mbalimbali kwenye jamii, na pia mawaziri wakuu wastaafu ambao hawagombei kwenye nafasi hiyo ili mradi tu apatikane mtu makini kwenye nafasi nyeti kama hii ya urais," alisema mstaafu mmoja aliyenukuliwa.
Chanzo cha Habari na Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment