NJOMBE

NJOMBE

Tuesday, January 24, 2012

Mdaktari waanza mgomo nchi nzima

JUMUIYA ya madaktari nchini, imetangaza mgomo utakaoanza leo nchi nzima hadi hapo serikali itakaporidhia kulipa madai yao ndipo madaktari watakaporudi kuendelea na kazi.
Akitangaza mgomo huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Madaktari, Dk. Ulimboka Stephen, alisema mgomo huo utakuwa wa nchi nzima kwa madaktari kutotoa huduma.
Alisema kuwa madaktari wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu hali ambayo wanashindwa kutoa huduma bora kutokana na kuwa na malipo finyu ya utendaji wao wa kazi.
“Sisi tumeazimia kugoma na hatutaki daktari yeyote aende kutoa huduma kwa wagonjwa mpaka hapo serikali itakaporidhia madai yetu ambayo kila siku yamekuwa yakipuuzwa,” alisema Dk. Stephen.
Aliongeza kuwa katika madai hayo wanaitaka serikali iboreshe mazingira ya kazi kwa wafanyakazi katika sekta ya afya pamoja na wagonjwa katika hospitali zote nchini.
Dk. Stephen alisema kuwa madai ya madaktari yamekuwa yakiipuzwa na baadhi ya watendaji serikalini kwa kupotosha wananchi kwa masilahi ya kuwaumiza wagonjwa walioko hospitalini.
Alisema katika madai mengine, wanataka nyongeza ya mshahara kutokana na kuwa hii wanayolipwa sasa haikidhi mahitaji ya kuendesha maisha yao, hatua inayowafanya kuhangaika kuhudumia katika hospitali zingine ili kuweza kukabiliana na mahitaji.
Wanadai nyongeza ya kulala kazini kutoka sh 10,000 hadi kufikia asilimia 10 ya mshahara wao sanjari na bima ya afya kwa kupewa kadi ya kijani ambayo inatambulisha juu ya kuweza kuhudumiwa.
Alisema kuwa katika mazingira ya kazi yao wanahitaji kukopeshwa magari ili kuweza kuwafikia wagonjwa kwa muda mwafaka.
“Serikali irudishe madaktari walio katika mafunzo bila ya kuwepo masharti yoyote kwa ajili ya kuwaandaa kwenda kutoa huduma bora kwa Watanzania,” alisema Dk. Stephen na kuongeza kuwa kutokana na kufanya kazi katika mazingira hatarishi, wanahitaji serikali iwape asilimia 30 ya mshahara baada ya kupata madhara wakati wa utoaji huduma.
Juzi, uongozi wa Chama cha Madaktari (MAT), ulishindwa kwenda na madaktari wanafunzi ‘intens’ kwenye mkutano wao na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Lucy Nkya.
Msemaji wa wizara hiyo, Nsachris Mwamwaja, alisema mkutano huo uliitishwa baada ya MAT kukwama kuonana na Waziri Mkuu na kutakiwa kurudi katika meza ya majadiliano na wizara hiyo.
Mwamwaja alisema kikao hicho kilichofanyika mchana wizarani hapo, ilibidi kuacha kujadili suala la wanafunzi hao na badala yake ikajadili malalamiko mengine yanayowasibu madaktari kwa ujumla.
Aliyataja matatizo hayo kuwa ni pamoja na madaktari kupewa nyumba, kuongezewa posho na mazingira magumu ambayo wamekuwa wakifanyia kazi.
Katika kikao hicho, Mwamwaja alidai kuwa iliamriwa kwamba suala la interns lingejadiliwa jana baada ya MAT kufika na wanafunzi hao lakini kabla ya muda uliopangwa kufika, chama hicho kiliifahamisha wizara kwamba wanafunzi hao wamekataa.
Kutokana na hali hiyo, Mwamwaja aliahidi kuwa jana angetoa taarifa ya mazungumzo yaliyojiri katika kikao hicho cha juzi, ikiwemo maamuzi waliyoafikiana kati ya MAT na wizara lakini hakufanya hivyo.
Habari na Chalila Kibuda

No comments:

Post a Comment