NJOMBE

NJOMBE

Tuesday, January 31, 2012

Lowassa, familia wachangia KKKT Simiyu mil. 21/-

KANISA la Kiinjili na Kilutheli Tanzania (KKKT), linalotarajia kuanzisha Dayosisi mpya ya Shinyanga na Simiyu limefanikiwa kukusanya Sh milioni 116 taslimu ambapo kati ya hizo, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na familia yake walichangia Sh milioni 21.

Katika harambee hiyo, Mchungaji wa KKKT, Philbert Celestine alimshukuru Lowassa na familia yake pamoja na wageni waalikwa kwa kufanikisha mchango huo ambao ulivuka lengo.

Awali, harambee hiyo ilikuwa na lengo la kupata Sh milioni 114 ili kukamilisha ujenzi wa kanisa hilo lakini walifanikiwa kuvuka lengo na kupata Sh milioni 204, kati ya hizo fedha
tasilimu zikiwa ni Sh milioni 116.

Akisoma risala kwa niaba ya KKKT Dayosisi ya Mashariki ya Ziwa Victoria, Mchungaji Celestine alisema kuwa kanisa hilo jipya likimalizika na kuifikia malengo waliyojiwekea,
litasaidia katika kukuza ufahamu wa kiroho baina ya waumini wa dayosisi hiyo mpya ambayo inatarajia kufunguliwa mapema mwaka 2013.

Alisema lengo lao ni kuwafikia na kupanua huduma ya neno la Mungu kwa kuwajenga waumini hao hasa ukizingatia Mkoa wa Shinyanga unaongoza kwa mauaji ya vikongwe na watu wenye ulemavu wa ngozi (albino).

Kwa upande wake, Lowassa akizungumza waumini hao, alisema kuwa suala la ujenzi wa makanisa nchini ni zuri na ni vema kwa sasa kutokuwategemea wafadhili kama ilivyokuwa awali na badala yake tubadilike kwa kujenga sisi wenyewe.

“Zamani tulikuwa tumezoea kujenga makanisa kwa kuwategemea wafadhili mbalimbali kutoka nje ya nchi hasa wazungu, lakini kwa sasa tubadilike tujenge wenyewe kwani uwezo tunao wa kuchangishana,” alisema Lowassa.

Lowassa alisisitiza kuwa yeye yupo tayari kurudi akiitwa katika harakati zozote za kuchangia ujenzi wa nyumba za ibada. Askofu wa Dayosisi ya Mashariki ya Ziwa Victoria, Andrea Gule akitoa shukrani zake katika harambee hiyo, aliwataka wananchi na waumini kwa ujumla kuwa na moyo wa kuthubutu katika kuchangia ujenzi hasa wa nyumba za ibada ili kuwakomboa
watu kiroho.

No comments:

Post a Comment