NJOMBE

NJOMBE

Sunday, September 16, 2012

Ghasia zaidi mgodini Afrika Kusini

Polisi wa Afrika Kusini

Polisi wa Afrika Kusini
Kumekuwa na ghasia zaidi katika mgodi wa Marikana nchini Afrika Kusini ambako polisi wametumia gesi ya kutoa machozi na risasi za mpira kuwatawanya wafanyakazi wa mgodi huo ambao wamekuwa wakiandamana magharibi mwa mji mkuu wa Pretoria.
Polisi hao walivamia makazi ya wafanyakazi hao mapema asubuhi siku ya Jumamosi wakikamata silaha mbalimbali zikiwemo mapanga na mikuki.
Serikali ya Afrika Kusini imeapa kukomesha migomo katika machimbo ya migodi nchini humo.
Migomo hiyo imekuwa ikisambaa na kuendelea tangu polisi walipowaua wachimba migodi 34 katika mgodi wa Marikana hapo Agosti 16 mwaka huu.
Siku ya Ijumaa baraza la mawaziri lilitangaza kuwa halitavumilia kile walichokiita mikutano isiyo halali na kutishia kuwanyanganya silaha waandamanaji hao.

Moto

Wanaume kwa wanawake na watoto walitawanyika baada ya polisi waliokuwa wakisaidiwa na helikopta za jeshi zilizokuwa angani zikirusha risasi za mpira na gesi za kutoa machozi kwa waandamanaji.
Maombolezo wakati wa mazishi ya wachimba madini waliouawa
Picha za televisheni zilionyesha watu waliokua na majeraha yaliyochuruzika damu.
"Gari la polisi lilitupita, tulikuwa ni kundi la wanawake na watu wengine walikimbia. Nilisimama pale nikiangalia na walinipiga risasi mguuni," Melita Ramasedi aliliambia shirika la habari la Sapa.
Wakati polisi wakiwasili katika eneo hilo waandamanaji walitumia matairi yaliyowashwa moto kuzuia polisi hao kuingia katika eneo hilo, ripoti zinasema.
Mapema polisi 500 walifanya uvamizi wa makazi ya wafanyakazi hao mapema asubuhi wakikamata silaha mabalimbali, msemaji wa polisi Thulani Ngubane amesema.
Ameliambia shirika la habari la AFP kuwa polisi waliwakamata watu 12 ingawaje watano kati yao ni kwa makosa ya kukutwa na madawa ya kulevya na sio silaha.
"Popote tutakapoana tabia kama hii ya vurugu na watu wakijichukulia sheria mikononi kwa kufanya maandamano yasiyo halali, hakika tutachukua hatua," alisema.
"Polisi hawatasita kuchukua hatua. Tutachukua hatua kama ambavyo tumekwisha anza na tutaendelea kufanya hivyo."
Maandamano hayo yameshuhudia mamia ya wafanyakazi wakiwa na fimbo na mapanga wakipita kutoka mgodi mmoja hadi mwingine eneo la Marikana na maeneo mengine na kutishia yeyote atakayerejea kazini.

Malipo yakataliwa

Wafanyakazi hao wamekuwa wakidai nyongeza ya mishahara kufikia randi 12,500 kwa mwezi (sawa na pauni 930 au dola za kimarekani 1,500) kutoka kiwango cha sasa cha kati ya randi 4,000 hadi 5,000.
Mapambano kati ya polisi na waandamanaji hivi Karibuni
Mapambano kati ya polisi na waandamanaji
Siku ya Ijumaa wafanyakazi hao walikataa ahadi ya nyongeza ndogo ya mishahara, ya randi 1,000 kwa mwezi, iliyotolewa na mwajiri wao kampuni ya Lonmin,wakisema kuwa ni sawa na kuwatukana.
Tokea vifo vya mwezi Agosti katika mgodi wa Marikana, migomo imekuwa ikisambaa katika maeneo mengine ya migodi nchini Afrika Kusini.
Waziri wa fedha Pravin Gordhan ameonya kuwa migomo hiyo inaweza kuathiri ukuaji uchumi, ajira na imani ya wawekezaji katika nchi hiyo yenye uchumi mkubwa barani Afrika.
Baadhi ya vyama vya wafanyakazi vimetishia kuitisha mgomo mkubwa.

No comments:

Post a Comment