NJOMBE

NJOMBE

Sunday, September 2, 2012

Vigogo waiweka CCM njiapanda

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kipo njiapanda, baada ya vigogo wake ambao ni wabunge, kuamua kuchukua fomu za kuwania uongozi ndani ya chama hicho, katika ngazi ya wilaya, kinyume cha kanuni za uchaguzi.
Marekebisho ya katiba yaliyofanywa na chama hicho katika kikao chake cha Februari 12, mwaka huu yanawazuia wabunge kugombea nafasi za uongozi ndani ya chama katika ngazi ya wilaya kama hatua ya kutoa fursa kwa wanaCCM wengine kujaza nafasi hizo za uongozi.
Kwa mujibu wa marekebisho hayo, mbunge ataruhusiwa kugombea nafasi za uongozi wa chama ikiwa atapewa kibali cha Kamati Kuu (CC). Pia  itafanya hivyo kwa kuzingatia mazingira maalumu ya maombi yatakayowasilishwa na kamati ya siasa ya wilaya au mkoa.
Mabadiliko hayo, pia ndiyo yaliyohamishia ujumbe wa NEC kutoka katika ngazi ya mkoa kwenda wilaya, uamuzi ambao umeanza kutekelezwa katika mchakato wa uchaguzi unaoendelea hivi sasa.
Hata hivyo, kipengele hicho cha katiba ambacho kupitishwa kwake kulipata upinzani mkubwa kutoka kwa wabunge wa chama hicho, kinaonekana kupuuzwa kutokana na wengi wao kujitokeza, wakiwamo mawaziri na kuchukua fomu za kugombea uongozi kinyume cha katiba ya chama chao.
Miongoni mwa vigogo waliochukua fomu ni aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika na Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk Abdallah Kigoda, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk Mary Nagu na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi.
Wengine ni Wabunge Deo Filikunjombe(Ludewa), Mussa Azzan Zungu (Ilala), Dk Hamis Kigwangalla (Nzega ), Andrew Chenge (Bariadi Magharibi), Godfrey Zambi (Mbozi Magharibi), Seleman Nchambi (Kishapu), Luhaga Mpina (Kisesa), Dk Titus Kamani (Busega), Andrew Chenge (Bariadi Magharibi), John Komba Mbinga Magharibi, James Lembeli (Kahama), Ahmed Salum (Solwa).
Habari kutoka ndani ya chama hicho zinaeleza kuwa suala hilo tayari limeanza kuwaumiza vichwa vingozi wa CCM, kutokana na wingi, pia aina ya wabunge walioamua kuingia katika kinyang’anyiro ilhali mazingira ya kugombea kwao yakithibitisha kutokuwapo kwa udharura.
“Ni kweli kwamba tupo njiapanda kwa sababu hapa chama lazima kiamue ama kufuata kanuni au kutumia mwanya uliowekwa kuwaruhusu wote wagombee, lakini hata kikifanya hivyo maana ya marekebisho hayo haitakuwepo,” alisema mmoja wa watoa habari wetu ndani ya CCM na kuongeza:
“Wewe fikiria ikiwa kwa mfano watamkatalia mtu kama Lowassa, Profesa Mwandosya au Mkuchika (George), hilo unadhani linawezekana? Hapo si watakuwa wanatafuta ugomvi tu.”
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu suala hilo, hakuwa tayari kulizungumzia akisema, bado ni mapema mno kwani kuna vikao vingi vya chama kabla majina ya wagombea kuwasilishwa mbele ya vikao vya juu ambavyo ni CC na NEC.
“Mimi nadhani bado ni mapema, ijapokuwa ni kweli kwamba tulipitisha mabadiliko hayo, lakini naamini kamati husika katika ngazi za mikoa na wilaya zinafahamu wajibu wake. Kama hivyo ndivyo, basi tusubiri majina yakifikishwa kwetu ndipo tunaweza kutoa tamko.

Wabunge hawajui mabadiliko

Baadhi ya wabunge waliochukua fomu kugombea walisema, wamefanya hivyo kwani wanavyofahamu, kanuni bado hazijabadilika na kwamba kilichopo ni mapendekezo ambayo hadi sasa bado hayajapitishwa na vikao husika.
Filikunjombe alisema: “Kwanza ninavyofahamu, kanuni na katiba havijabadilishwa kwani yalikuwa ni mapendekezo tu, kwa hiyo hakuna kinachotuzuia sisi wabunge kugombea. Pili niseme kwamba jambo lolote linalogusa wabunge, linapaswa kujadiliwa na kupata mwafaka katika vikao vya chama”.
Kwa upande wake, Zungu alisema CCM hakikuwahi kupitisha azimio la kuwakataza wabunge kugombea nafasi mbalimbali kwenye chama hicho.
Alisema ni haki ya mwanachama yeyote kuchagua au kuchaguliwa na kwamba wabunge wanaruhusiwa kugombea nafasi yoyote kwenye chama… “Sijawahi kusikia kitu kama hicho katika CCM, ni ruksa kugombea nafasi mbalimbali ikiwa vikao vitakupitisha.”
Dk Kigwangalla alisema, anakumbuka liliwahi kutolewa wazo la kuwazuia wabunge kugombea nafasi kwenye chama lakini halikupitishwa na NEC… “Halikupitishwa wazo hilo hivyo wabunge wanaruhusiwa kugombea nafasi za uongozi kwenye chama. Hakuna kizuizi chochote.”

Mabadiliko ya Katiba

Katika kikao chake cha Februari 12, mwaka huu Nec ilipitisha mabadiliko ya katiba kwa kuzifanya nafasi za ujumbe wa Nec na wenyeviti wa wilaya na mikoa, kuwa ni kazi za muda wote kwa lengo la kuwaweka viongozi hao kuwa karibu na wanachama na kushughulikia matatizo yao.
Kwa kuzingatia mabadiliko hayo, ni dhahiri kwamba wabunge na madiwani hawezi kuwania nafasi za uongozi ndani ya chama, kwani wanazuiwa na Kanuni ya Uchaguzi ya CCM, toleo la Februari, 2010.
Kifungu cha 22 cha kanuni hiyo kinasema: Mwanachama ambaye anaomba nafasi ya uongozi ambayo ni kazi ya muda wote, hataruhusiwa kushika nafasi ya aina hiyo zaidi ya moja katika chama isipokuwa Kamati Kuu imeamua vinginevyo.
Pia, Kifungu cha 23 kinataja nafasi za uongozi za muda wote kuwa ni mwenyekiti wa tawi au mtaa, mwenyekiti wa kata au wadi, mwenyekiti wa jimbo au wilaya, mwenyekiti wa mkoa, makatibu wa halmashauri kuu wa ngazi zinazohusika, diwani, mwakilishi na mbunge.
Uamuzi wa Nec kuongeza nafasi wajumbe wa wilaya katika orodha ya nafasi za muda wote, uliwaengua wabunge, wawakilishi na madiwani kugombea nafasi ndani ya chama.
Hata hivyo, wabunge na wawakilishi hawakuzuiwa kugombea nafasi za Nec katika viti 10 vya Tanzania Bara na Visiwani au katika jumuiya za chama hicho ambazo ni Wazazi, UWT na UVCCM.
Katika marekebisho hayo, wajumbe wa Nec watakuwa  ni wajumbe 10 kutoka Tanzania Bara, 10 kutoka Zanzibar, 10 wa kuteuliwa na Mwenyekiti wa CCM, wajumbe wanaoingia kwa nafasi zao, wajumbe 221 wanaochaguliwa kutoka wilayani na wanaotoka kwenye vyombo vya uwakilishi; wabunge 10 na wawakilishi watano.
Wengini ni wajumbe kutoka jumuiya za chama; wanaochaguliwa na UWT 15, UVCCM 10 na Wazazi watano.
Wakati marekebisho hayo yakiwa bado ni mapendekezo, wabunge wa CCM walianzisha mpango wa kuyapinga, lakini walipokutana na Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, mjini Dodoma waligeuka mabubu na kushindwa kuzungumzia.
Miongoni mwa malalamiko hayo, yalikuwa ni kwamba marekebisho ya Katiba hayakuwashirikisha wakiwa ni wadau na kwamba kwa kufanya hivyo, kulikuwa na lengo baya la kuwaengua kushiriki shughuli za chama.

Taarifa hizo ziliwanukuu wabunge hao wakidai kuwa suala hilo, linahitaji mjadala wa kitaifa ili kutoa wigo mpana kwa wanachama kutoa mawazo yao. Hata hivyo, baadaye CC na Nec walipitisha mabadiliko hayo ambayo yanapaswa kuzingatiwa katika uchaguzi wa sasa.
Chanzo ni Mwananchi

No comments:

Post a Comment