NJOMBE

NJOMBE

Saturday, September 1, 2012

Rais mpya wa Ghana kuwakilisha chama

Rais John Mahama
Chama tawala nchini Ghana, NDC, kimemteua rais mpya John Mahama kuwa mgombea wake wa urais katika uchaguzi utakaofanyika mwezi Disemba mwakani.
Bwana Mahama alichukua hatamu za uongozi baada ya kifo cha marehemu rais John Atta Mills.
Atta Mills, aliyeugua saratani ya koo , alikuwa ameitawala Ghana tangu mwaka 2009 na alitarajiwa kugombea tena urais kwa muhula wa pili.
Ghana imesifiwa sana kwa namna ilivyoweza kukabidhi mamlaka bila fujo baada ya kifo cha Mills.
Wadadisi wanasema kuwa wengi wanaitazama Ghana kama mfano mzuri wa nchi yenye demokrasia barani Afrika licha ya kujulikana kwa siasa zake kali.
Bwana Mahama, aliyehudumu kama makamu wa rais wa marehemu Mills, atapambana na Nana Akufo-Addo wa chama cha New Patriotic Party na ambaye alishindwa katika duru ya pili ya uchaguzi wa Disemba mwaka 2008 kwa asilimia ndogo sana.
Kulingana na taarifa za vyombo vya habari nchini humo, Mahama alishinda zaidi ya asilimia 99 ya kura zilizopigwa katika kongamano la chama tawala ambalo linafanyika mjini Kumasi.

No comments:

Post a Comment