NJOMBE

NJOMBE

Friday, September 7, 2012

Wachimba migodi waachiliwa huru

Wachimba migodi waachiliwa
Karibu wafanyakazi wote wa migodi ya madini nchini Afrika Kusini waliokamatwa katika vurugu za mwezi uliopita wameachiliwa.
Watu arobaini na wanne waliuawa katika vurugu hizo zilizowahusisha polisi na wafanyakazi wa migodi ya madini ya dhahabu ya Marikana.
Hatua hiyo imekuja wakati vyama vingi vya wafanyakazi wa migodi vimetiliana saini na kampuni ya migodi kumaliza mgomo ambao umeathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya machimbo ya platinum.
Lakini makubaliano hayo hayakutiwa saini na chama muhimu kisichotambuliwa, ambacho ni kitovu cha mgogoro huo.
Kutoka katika vilima kuzunguka mji wa Rustenberg unaweza kuona machimbo yaliyosambaa, yakiwa yamezungukwa na kambi za maskwota, ambamo wanaishi wafanyakazi wa migodi hiyo na familia zao.
Hapa ndipo inapotoka asilimia sabini na tano ya madini ya dhahabu nyeupe ijulikanayo kama platinum inayozalishwa duniani.
Chama chao cha Taifa cha Wafanyakazi wa Migodi, kinachotambuliwa kisheria, kinaonekana kuwa karibu karibu sana na kampuni iliyosajiliwa Uingereza ya Lonmin.
Pia kinaonekana kuwa karibu zaidi na Rais Jacob Zuma. Kwa hiyo wafanyakazi wameelekeza macho yao kwa chama cha AMCU - chama ambacho hakitambuliwi na kampuni hiyo.
AMCU ilikuwa katika mazungumzo ya siku nzima hapo jana, yaliyosuluhishwa na makanisa na serikali. Lakini makubaliano yalipofikiwa wajumbe wa chama hicho cha AMCU walitoka nje. Kitu walichotaka ni kuboresha malipo yao na hakuna la kujadili zaidi.
Malalamiko yao yamechukuliwa na Julius Malema, ambaye alifukuzwa kutoka chama cha ANC wakitafuta mahali pa kusimamia malalamiko yao.
Na vikundi vingine vya mrengo wa kushoto vinawaunga mkono wachimba migodi hao.Lakini bei ya madini ya platinum ambayo imekuwa ikianguka kwa asilimia ishirini kwa mwaka mmoja uliopita, kampuni hiyo inasema haina uwezo wa kuwalipa zaidi wafanyakazi wa migodi hiyo.

No comments:

Post a Comment