NJOMBE

NJOMBE

Saturday, March 17, 2012

Lema aomba kesi itupwe

MBUNGE wa Arusha Mjini, Godbless Lema, jana aliiomba mahakama kutupilia mbali tuhuma dhidi yake kwa sababu ni za uwongo, chuki na fitna.

Amedai kuwa hali hiyo ndiyo iliyowafanya Waziri mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowasa na aliyekuwa mgombea kupitia CCM, Dk Batilda Burian, hawakufika mahakamani kutoa ushahidi  licha ya kutajwa mara kadhaa.
Akiongozwa na wakili wake, Method Kimomogoro katika kutoa ushahidi, Lema alidai kuwa kesi hiyo iliyofunguliwa na wapiga kura watatu, imetokana na chuki za mlalamikaji wa kwanza, Mussa Mkanga  baada ya kukosa udiwani katika Kata ya Sombetini.
Alimwomba Jaji Gabriel Rwakibarila kuwaamuru wadai kumlipa ghrama zote alizoingia na  muda wake aliopoteza tangu alipoanza kuhudhuria shauri hilo lililoanza kuunguruma Julai mwaka jana, ili iwe fundisho kwa watu wengine.

Alimweleza jaji kuwa kwa kipindi cha  miezi mitatu sasa ameshindwa kutekeleza majukumu yake ya kibunge, kwa sababu ameazimika kuhudhuria mahakamani kushughulikia kesi hiyo.

Alidai kuwa kesi hiyo imetokana na madai ya uwongo uliotungwa na wadai Mkanga  na wenzake Agnes Mollel na Happy Kivuyo wanaowakilishwa na mawakili Alute Mughwai na Modest Akida.

Aliieleza mahakama kuwa kama tuhuma dhidi yake zingekuwa za ukweli, Lowasa na Dk Burian waliotajwa kwa namna ya kuonekana kudhalilishwa na kushushiwa  hadhi yao mbele ya jamii, wangefika mahakamani kutoa ushahidi ili kuthibitisha tuhuma dhidi yake.
Lema alidai viongozi hao wameacha kwenda mahakamani kutokana na ukweli kwamba maneno yanayodaiwa kuwa aliyatamka dhidi yao si ya kweli.

Alidai kuwa hiyo pia ndiyo sababu ya Dk Burian kutofungua kesi dhidi yake baada ya uchaguzi  mkuu uliopita.

Aliieleza mahakama iliyojaa wasikilizaji kuwa hata katika barua yake ya malalamiko kwa msimamizi wa uchaguzi, Dk Buriana alishindwa kuorodhesha au kutoa mifano ya kauli za matusi, kashfa na udhalilishaji alizodaiwa kuzitoa.
Lema alidai kuwa kitendo hicho ndicho kilichomlazimisha  msimamizi wa uchaguzi katika  Jimbo la Arusha Mjini, Raphael Mbunda kumruhusu kuendelea na kampeni.
Shahidi hiyo alidai hata vielelezo vya nakala ya CD zizodaiwa kurekodiwa maneno yake ya matusi hayakuwasilishwa mahakamani kuthibitisha tuhuma dhidi yake.

Alidai kuwa  CD hizo zingewasilishwa mahakamani kesi hiyo ingekuwa imeisha mapema kwa sababu  ukweli ungedhihirika.

Katika hatua nyingine, Jaji Rwakibarila aliendelea kuwavunja mbavu kwa vicheko wananchi wanaohudhuria mahakamani baada ya jana kuanza mtindo mpya ya kudhibiti wanaosinzia wakati kesi inaendelea kwa  kuwaamuru kusimama kwa dakika kadhaa kabla ya kuwaruhusu kuketi tena.
Habari na Mwananchi

No comments:

Post a Comment