NJOMBE

NJOMBE

Thursday, March 15, 2012

Nafasi ya mwanaume na baba katika maisha ya ndoa na familia

Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, ninapenda kuchukua fursa hii kukaribisha tena katika makala hii ya ndoa na familia. Juma lililopita tuliangalia kwa pamoja nafasi ya mwanamke na mama katika Familia. Tukahitimisha kwa kukumbusha kwamba, Bikira Maria, Malkia wa Familia ni mfano bora wa kuigwa kwani, kutokana na kuukubali mpango wa Mungu katika maisha yake, amekuwa ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu.
Leo tunaendelea kupembua kuhusu hati ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili kuhusu wajibu wa familia za kikristo katika ulimwengu mamboleo. Hati hii ya familiaris consortio no. 25 inasema katika muungano wa ndoa mume anaitwa pia kuwa baba katika familia yake.
Upendo wa kweli wa Wanandoa unadai mwanamume atambue kuwa mke wake ni msaidizi ambaye katika sura na mfano wa Mungu wako sawa sio mtumwa wake hivyo ampokee kwa upendo, kama zawadi na awe na shukurani kwa zawadi ya hii. Mfano wa upendo unaodaiwa kati yao ni kama ule wa Kristo kwa kanisa lake (Efeso 5:21-33)
Mwanamume anapaswa kuwa baba wa watoto kibalojia, kisaikolojia, kijamii na kiroho hivyo huyu ni mlezi halisi wa watoto wake katika nafasi yake. Mwana shairi mmoja analinganisha nafasi ya baba katika malezi ya watoto na mwalimu anayemfundisha mwanafunzi wake kuogelea. Anasema endapo mwalimu atamshikilia sana mwanafunzi kwa hofu ya kuzama basi mwanafunzi hatajifunza kuogelea kabisa.Lakini endapo atamwachia sana bila kumpa uangalizi katika maji basi mwanafunzi atazama.
Ndivyo ilivyo kwa baba endapo atakuwa mkali mno mtoto wake hataweza kujifunza kujitegemea kabisa kwani atashindwa kutumia uhuru wake. Lakini akimwachia tu bila kumwelekeza uhuru utazidi na mtoto wake atakuwa mtoto aliyekosa malezi ambayo ni hatari sana kwa makuzi yake.
Tujifunze nini katika hayo yote tuliyosema? Kwanza kila mmoja ajitahidi kuimarisha upendo kwa mwenzake katika nafasi yake.
Pili ni ukweli kwamba katika familia nyingi kuna kilio cha kutoweka kwa akinababa. Wapo akina baba ambao wamebaki baba wa uzazi tu lakini ukiwauliza kuhusu watoto wao watasema mama yao ndiye anajua. Na bahati mbaya zaidi wapo watoto ambao hata hawawafahamu baba zao. Tukumbuke mtoto aliyekosa malezi ya baba hupungukiwa mengi. Ni vizuri akina baba tujitahidi kumwiga Mt. Yosefu ambaye wakati wote alijitahidi kuwa karibu na mama Maria katika makuzi ya mtoto Yesu.
Tumalizie tafakari yetu kwa maneno ya Yoshua bin Sira sura ya 30 anayesema, Mzazi ampendaye mwanawe, atamrudi mara kwa mara ili amwonee fahari jinsi anavyokua...hata kama baba yake akiwa amekufa atakuwa kama hakufa maana ameacha nyuma mtoto anayefanana naye.
Kutoka Studio za Radio Vatican, mimi ni Padre Raphael Mwanga, toka Jimbo Katoliki Same, mwanafunzi wa ndoa na familia, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa, Laterano, Roma.
Ujumbe kutoka Radio Vatican.

No comments:

Post a Comment