NJOMBE

NJOMBE

Monday, March 12, 2012

Mkuu wa Mkoa Arusha akana hajatowa siri Chadema

PINGAMIZI lililowekwa na Chadema kwa mgombea ubunge wa CCM katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki mkoani Arusha, Siyoi Sumari, limezua utata baada ya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kudaiwa kuvujisha barua ya siri kwa chama hicho cha upinzani.

Vyanzo vya habari vya gazeti hili, vimeeleza kwamba barua hiyo ya siri ilivujishwa na kigogo mmoja wa Serikali mkoani hapa, kwa kile kinachodaiwa, chuki za kisiasa ambapo aliwaagiza makada wa CCM kuifikisha Chadema, ili Siyoi awekewe pingamizi.

Hata hivyo Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo alipoulizwa na mwandishi wa gazeti hili kwa njia ya simu jana, alikanusha vikali ofisi yake kuvujisha barua hiyo kwa Chadema, huku akisema kwamba Serikali imeanza uchunguzi wa kina kubaini Chadema walikoipata barua hiyo.

“Mimi kwanza situnzi nyaraka za Serikali na siwezi kutoa nyaraka za Serikali lakini ni lazima tuchunguze Chadema wameipata wapi hiyo document (waraka),”alisema Mulongo.

Chanzo cha mvutano

Juzi wakati Chadema wakitangaza uamuzi wa kumwekea pingamizi mgombea ubunge wa CCM, Sumari, walitumia barua iliyoelezwa kuwa ya siri, ambayo Mulongo aliandikiwa na Idara ya Uhamiaji mkoani hapa kuhusiana na utata wa uraia wa mgombea huyo.

Hata hivyo katika mchakato wa kura za maoni za CCM, Mulongo anadaiwa kuwa katika kundi lililokuwa likimpinga Sumari kupitishwa kugombea na chama hicho tawala.

Mkurugenzi wa Bunge na Halmashauri ya Chadema, John Mrema alisema kwamba barua hiyo yenye kumbukumbu namba AR/32/ VOL.1/85 iliyoandikwa na Mkuu wa Uhamiaji mkoani Arusha, Daniel Namomba kwenda kwa Mkuu huyo wa Mkoa, ilieleza taratibu mbalimbali za kisheria za mtu kuwa raia au la.

Katika barua hiyo iliyoandikwa Febuari 29 mwaka huu, Namomba alitoa ufafanuzi wa sheria hiyo kutokana na maombi ya kufanya hivyo aliyotakiwa na Mulongo kupitia barua yenye kumbukumbu namba CFAl18l114l01l20 .

Katika barua hiyo Mkuu huyo wa Idara ya Uhamiaji alieleza kwamba mgombea huyo alizaliwa eneo la Thika nchini Kenya Mei 11 mwaka 1979 na kwenda mbali zaidi kufafanua kwamba, kwa mujibu wa Sheria ya Uhamiaji  namba 7 ya mwaka 1995, kuna uraia wa aina tatu ambao ni wa kuzaliwa, kurithi na kuomba.

Ndani ya barua hiyo, Namomba alifafanua kifungu ambacho mtu anayezaliwa nje ya nchi kama atarithi uraia wa wazazi wake, mmoja au wote, ukomo wake ni miaka 18 na kama atakuwa amezaliwa nje ya nchi, na amefikisha miaka 18 anapaswa kuukana uraia alionao na kuomba uraia wa nchi ambayo anaishi kwa kuapa kiapo cha utii, jambo ambalo Idara hiyo haina kumbukumbu kama Siyoi aliukana uraia wa nchi alikozaliwa.

Kauli ya Mkuu wa Mkoa
Kufuatia utata wa sakata hilo, Mkuu huyo wa Mkoa alipoulizwa juu ya taarifa hizo, aliendelea kukanusha madai ya ofisi yake kuvujisha barua hiyo huku akisisitiza kwamba ana uhakika barua hiyo haijatokea ofisini kwake naye hahusiki kwa namna yoyote na kuvuja barua hiyo.

“Mimi nakwambia sihusiki kabisa na hilo jambo na nina uhakika kwamba hiyo barua, Chadema hawakuitoa ofisini kwangu, waulizeni Chadema wameitoa wapi ? ”Alihoji na kusisitiza Mulongo

Alikituhumu Chadema kuzua habari hiyo na kudai kwamba wakati fulani, waliwahi kuibuka na nyaraka ambazo wanadai walizitoa Idara ya mambo ya ndani na kumbe si kweli. Alisema ofisi yake itachunguza kwa kina kujua chama hicho kilikopata barua hizo.

Hata hivyo alipotakiwa kujibu madai kwamba ndiye aliyeagiza Idara ya Uhamiaji ichunguze uraia wa Siyoi, Mulongo alisema ni lazima watu wafahamu ya kwamba CCM ilihitaji vielelezo vya mgombea yeyote ambaye alikuwa na mashaka, ili vifikishwe mbele ya chama hicho.
Habari zaidi na Mwananchi

No comments:

Post a Comment