NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, July 11, 2012

KUELEKEA KATIBA MPYA NA SISI TUIGE YA UFARANSA NINI SOMA MAPINDUZI 1789


Mapinduzi ya Ufaransa ya mwaka 1789 yalikuwa aina fulani ya maasi ya wanaokandamizwa na kunyonywa, dhidi ya maisha duni, magumu na yasiyovumilia miongoni mwa wananchi.

Baadhi ya mambo yaliyochochea harakati na hatimaye mapinduzi, yaliyozaa moja ya katiba za kwanza bora kabisa duniani, ni pamoja na mazingira tete ya kisiasa, kijamii, kiuchumi na mchango wa wanaharakati wasomi walioiamsha jamii, kama inavyotokea leo hapa kwetu.


Serikali ya Ufaransa, ilijengeka juu ya utawala wa Mfalme mwenye mabavu (absolute monarch). Licha ya kukua kwa mawazo mapya na mwamko juu ya utawala bora na haki za binadamu, bado Mfalme alijiona ndiye chanzo cha mamlaka yote. Alizoea kujitapa kwa kusema: “Mimi ndiye Taifa, na Taifa ndilo mimi”.


Kufikia nusu ya pili ya karne ya 18, ufalme ulikithiri kwa rushwa, udhaifu mkubwa kiutendaji na Taifa kukosa mwelekeo.


Nchini Ufaransa, kila mwananchi aliwekwa kwenye kundi la kitabaka, maarufu kama estate. Tabaka la kwanza na la juu kabisa lilikuwa la makasisi wa kanisa, wakiwamo ma-askofu, maparoko na viongozi wengine wa kanisa. Hawa hawakuzidi 100,000 kwa idadi, katika nchi ya watu 25,000,000 wakati huo. Walikuwa na upendeleo maalumu katika jamii, kama vile kusamehewa kodi zote, kutoshitakiwa na walikuwa matajiri kupindukia.


Tabaka la pili lilikuwa la Wafaransa kutoka familia zenye nasaba bora na maarufu. Kama ilivyokuwa kwa wale wa tabaka la kwanza, hawa nao walikuwa matajiri, walisamehewa kodi; walishika nafasi za juu serikalini na jeshini. Waliposhitakiwa mahakamani, waliweza kuchagua wao wenyewe mahakimu wa kusikiliza na kuhukumu kesi zilizowakabili.


Tabaka la mwisho, lilikuwa tabaka la tatu lililojumuisha wananchi wengine wote, wakiwamo wafanyabiashara, wanasheria, madaktari, wakulima wa kati na wadogo na wafanyakazi.


Zaidi ya asilimia 80 ya Wafaransa waliishi vijijini kwenye vishamba vidogo vidogo kwa kuwa karibu ardhi yote ilimilikiwa na kanisa. Hawa walichakaa kwa kodi lukuki walizotozwa na serikali ambazo tabaka la kwanza na la pili hawakulipa.


Walitozwa kodi ya kanisa (tithe), ambayo ilikuwa moja ya kumi ya mapato yote, walitozwa kodi ya ardhi (taille) na walitozwa kodi ya kichwa (capitation).


Walilipa pia kodi ya mapato (vingtiene), kodi ya chumvi (gabelle ) na walijitoa nguvu kwa shuruti kujenga barabara za Mfalme kila wiki (corvee) na kodi nyinginezo.


Ukiangalia hali ilivyo nchini kwetu sasa ni kama tunapita njia hiyo ya matabaka kujengeka mithili ya Ufaransa ya kale, huku tabaka la mwisho, la wakulima na wafanyakazi likionja adha ya kodi lukuki na huduma duni lakini za gharama kubwa (maji, umeme, tiba, bei duni za mazao).


Kufikia mwaka 1788, jamii ya walalahoi iliuona utawala wa Mfalme Louis wa XVI kuwa usio na manufaa kwao na uliopitwa na wakati. Maswali matatu yalitawala katika jamii wakati huo: Ni kwa namna gani utawala huo wa mabavu ungefikia mwisho katika nchi isiyo na katiba? Namna gani tabaka hizo tatu zingeweza kushirikiana kuuondoa madarakani kwa njia ya kura? Tabaka hizo zitakaaje na kupiga kura?


Mei 5, 1789, Bunge Kuu la Ufaransa (The Estates General) la tabaka zote tatu, liliketi mjini Versailles, kuzungumzia namna ambavyo katiba ya nchi ingeweza kupatikana ili kukabiliana na madaraka makubwa ya Mfalme.


Wakati wabunge kutoka tabaka la tatu walitaka tabaka zote tatu zikae kwa pamoja na kupiga kura kila “kichwa” kura moja, tabaka mbili za kwanza, kwa kuhofu kuzidiwa kura na tabaka la tatu (lililokuwa na wawakilishi mara mbili ya tabaka mbili za kwanza) na kuhatarisha maslahi yake, zilitaka kila tabaka lipige kura peke yake na kutoa matokeo.


Kama tabaka la kwanza na la pili yangepiga kura juu ya kuwa au kutokuwa na katiba kwa lengo la kulinda maslahi yake, tabaka la tatu lingeshindwa kwa tabaka mbili kwa moja (2 – 1). Hapo bunge likaendelea kukaa bila suluhu juu ya jambo hili.


Baada ya kuchoshwa na udhalimu wa tabaka la kwanza na la pili; Juni 17, 1789, wabunge wa tabaka la tatu walichukua uamuzi mgumu: walijitangaza kwa nguvu kuwa wao ndio bunge pekee la Ufaransa.


Huku wakiwa wamefungiwa milango wasiingie bungeni, wabunge hao walikusanyika kwenye kiwanja cha mpira na kuapa kutotawanyika hadi hapo watakapoipatia Ufaransa katiba. Kiapo hiki maarufu kinajulikana kama The Tennis Court Oath. Hapa Mapinduzi ya Ufaransa yakawa yamekwishaanza.


Kuona hivyo, na kwa hofu kuu juu ya nguvu ya umma kuanza kufanya kazi yake, Mfalme Louis wa XVI aliitisha haraka kikao cha tabaka zote tatu na kuagiza zikae na kupiga kura kila tabaka kivyake; lakini tabaka la tatu na baadhi ya wabunge kutoka matabaka mawili ya kwanza, walikataa kutii amri.


Mmoja wa wabunge wa tabaka la tatu, Count Mirabbeau, alisimama na kunguruma: “Tupo hapa kwa matakwa ya watu; ni singe (bunduki) pekee zitakazotutoa hapa, vinginevyo hatutoki”.


Kwa ushauri wa mke wake Marie Antoinnete, Mfalme Louis wa XVI alituma jeshi kuvunja bunge. Lakini, kwa mshangao wa kila mtu, askari walipofika eneo walipokusanyika, walitupa silaha na kuungana na “waasi” hao, huku ghasia na maandamano yakizidi kupamba moto mitaani kuwaunga mkono. Siku mbili baadaye, viongozi wa dini na wale wenye nasaba bora, waliungana na walala hoi hao.


Juni 27, 1789, huku akiwa amejawa hofu, Mfalme Louis wa XVI alisalimu amri na kuagiza wabunge wa tabaka zote tatu kukutana. Kufikia hapo, kile kilichoanza kama bunge lililoitishwa kushauri tu, lilikuwa limegeuka kuwa serikali ya kitaifa.


Wakati bunge la umoja wa kitaifa likijadili nini cha kufanya, mmoja wao kutoka tabaka la wenye “nasaba bora” alitoa mawazo kwamba, “wakulima walikuwa wakiasi dhidi ya ukandamizaji, na kwamba, badala ya kwenda kinyume nao, bunge lipambane na udhalimu huo”.


Agosti 4, 1789, bunge lilifuta maslahi na marupurupu yote manono ya tabaka mbili za kwanza. Na kama hatua ya kwanza kwa kazi ya kuandika katiba, bunge (au bunge la katiba kama lilivyokuja kujulikana) lilitoa azimio juu ya haki za binadamu na za raia.


Azimio hilo liliweka misingi mikuu ya serikali ambayo katiba iliyotarajiwa ilitakiwa kuzingatia, kama ifuatavyo:


Kwanza: Binadamu huzaliwa na kubakia huru na mwenye haki sawa.


Pili: Haki hizo ni haki asilia na ni pamoja na uhuru wa mtu binafsi, umiliki wa mali, usalama na haki ya kukataa kukandamizwa.


Tatu: Sheria ni kielelezo cha matakwa ya wananchi. Kila raia ana haki kushiriki yeye mwenyewe, au kupitia wawakilishi (wabunge) wake katika kuzitunga.


Nne: Mtu asituhumiwe, asikamatwe au kufungwa ila kwa kushitakiwa kwa kuzingatia matakwa ya sheria.


Chini ya azimio hili, mambo kama uvumilivu wa kidini, uhuru wa kujieleza na uhuru wa vyombo vya habari, yalitajwa kuwa moja ya mihimili ya uhuru wa mtu na kwa serikali yenye uhalali wa kutawala.


Septemba 1791, katiba iliyokuwa ikisubiliwa kwa hamu na wananchi, ilikamilika. Ilitoa na kufafanua kwa mara ya kwanza katika historia, mgawanyo wa madaraka kati ya utawala, bunge na mahakama. Kazi ya kutunga sheria ilikabidhiwa kwa bunge.


Jambo moja lisilo la kawaida lililofanywa na bunge hilo la katiba ni kwamba, baada ya kukamilisha kazi yake na kabla ya kujivunja, lilitangaza wajumbe wake kutostahili kugombea ubunge wa bunge jipya.


Katiba ni mapambano; haiji kwa ridhaa ya watawala. Mfalme Louis wa XVI alijaribu kuligawa Bunge ili lisipate muafaka juu ya katiba wakilishi kwa ajili ya wananchi wote ili kumwezesha kuendeleza udikteta wake kwa manufaa yake na maswahiba wake. Bila nguvu ya umma wa wanyonge, inayoshinda nguvu ya mtutu wa bunduki, Ufaransa isingepata Katiba bora na yenye kuzingatia utawala wa sheria na haki za binadamu. Baada ya hapo, dunia yote, hadi sasa, iliiga katiba hiyo ya Ufaransa.


Yaliyotokea na yanayotokea hapa nchini kuhusu historia ya michakato ya katiba hayatofautiani na yaliyotokea Ufaransa.

No comments:

Post a Comment