NJOMBE

NJOMBE

Wednesday, April 4, 2012

Polisi aliyetinga disko na bangi afukuzwa kazi

Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Absalom Mwakyoma
Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro, limemfukuza kazi askari wake, Deogratius Chang’a, kwa kosa la kuingia ukumbi wa disco wa Pub Alberto wa mjini hapa na kufanya vurugu, kuumiza watu na kukutwa na misokoto mitatu na nusu ya bangi.

Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Absalom Mwakyoma, alithibitisha jana kufukuzwa kazi kwa askari huyo na kueleza kuwa ni baada ya Mahakama ya kijeshi kumkuta na hatia na kuamuru afukuzwe kazi kwa fedheha.
Alisema kuwa kosa la kwanza la askari huyo ni kufanya fujo katika ukumbi huo na kumjeruhi mmoja wa wafanyakazi wa ukumbi huo kwa kumng’ata meno na kosa la pili ni kukutwa na misokoto ya bangi mfukoni.
“Mnamo Machi 24, mwaka huu, saa 6:05 usiku, katika kituo cha Polisi Kati Moshi Mjini, askari huyo alipekuliwa na kukutwa na bangi, kitendo ambacho ni kinyume na mwenendo mwema wa Jeshi la Polisi
Tanzania. Amepatikana na hatia kwa makosa yote mawili, Kamati ya Maadili ya Polisi ilipendekeza afukuzwe kazi kwa fedheha, hivyo tumemfukuza kazi kuanzia Aprili 3, mwaka huu,” alisema.
Askari huyo alimjeruhi mlinzi wa pub hiyo, Rajab Hamad, kwa kumng’ata meno mkononi, kutoa matusi na kuwapiga ngumi watu mbalimbali bila sababu, kitendo ambacho ni kinyume na mwenendo mwema wa Jeshi la Polisi nchini.
Baada ya tukio hilo, Jeshi hilo lilieleza kuwa  askari huyo akiwa amevalia kiraia alifika katika ukumbi huo kwa lengo la kucheza miziki na kwamba alikuwa akinywa pombe, lakini baada ya muda alianza kufanya vurugu.
Walinzi wa ukumbi huo walipojulishwa juu ya vurugu hizo, walifika na kuanza kukabiliana naye na ndipo alipomjeruhi mmoja kwenye mkono na mmiliki wa ukumbi huo, Christopher Shayo, alipoingilia kusuluhosha, alipigwa ngumi ya usoni.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment